1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yawashtaki watu 5 kwa njama ya kuiangusha serikali

23 Januari 2023

Waendesha mashtaka nchini Ujerumani wamewafungulia mashtaka ya uhaini watu watano wanaodaiwa kupanga njama ya kumteka Waziri wa Afya Karl Lauterbach, na walikuwa wamejiandaa kumuuwa ili kuiangusha serikali ya Ujerumani.

https://p.dw.com/p/4Mazm
Berlin PK Gesundheitsminister Lauterbach zu Cannabis-Legalisierung
Picha: MICHELE TANTUSSI/REUTERS

Kundi hilo lililoundwa katikati ya mwezi Januari 2022, lilijiwekea lengo la kuzusha mazingira kama ya vita vya wenyewe kwa wenyewe Ujerumani kwa mbinu za machafuko likiwa na matumaini ya kuiangusha serikali na demokrasia ya bunge. 

Waendesha mashtaka wamesema washukiwa hao walifanya maandalizi ya kina na kutengeneza matawi mawili ya kundi lao, moja la kijeshi na jingine la kiutawala.

Katika mpango wenye hatua tatu, walitaka kusababisha kukatika kwa umeme nchi nzima, kumteka Waziri wa Afya Karl Lauterbach, kuwauwa walinzi wake kama ingehitajika, na kisha kuitisha mkutano wa kuiondoa serikali na kumteuwa kiongozi mpya.