1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani: Seehofer asema hana shida tena na Merkel

Daniel Gakuba
8 Julai 2018

Waziri wa ndani wa Ujerumani Horst Seehofer, amesema mvutano mkali uliokuwepo kati yake na Kansela Angela Merkel kuhusu sera ya wahamiaji, sasa ni historia, na lililo muhimu sasa ni kutazama mbele.

https://p.dw.com/p/312fL
Merkel und Seehofer  bei CDU/CSU-Fraktionssitzung
Horst Seehofer (kushoto) na Kansela Angela MerkelPicha: Reuters/H. Hanschke

Kulingana na mazungumzo aliyoyafanya na gazeti la Bild am Sonntag la hapa Ujerumani, Horst Seehofer amesema viongozi wa vyama vinavyounda serikali ya Ujerumani, hivi sasa wanatazama mbele, wakiziacha nyuma tofauti kuhus sera ya wahamiaji iliyotishia kuisambaratisha serikali hiyo.

Amesema viongozi hao walikubaliana kuwakataa wahamiaji ambao wameshaomba hifadhi katika nchi nyingine za Ulaya, kupitia mikataba na nchi nyingine ambayo bado haijasainiwa.

Seehofer aliyetaka hatua thabiti zaidi, ameliambia Bild am Sonntag kuwa makubaliano hayo yanawasilisha ishara kwa ulimwengu mzima kuwa uhamiaji haramu haufai.

Yaliyopita si ndwele

Alipoulizwa juu ya uhusiano wake na Angela Merkel amesema, yaliyopita si ndwele, na kwamba muhimu ni yaliyoko mbele.

Migranten in Spanien gerettet
Suala la wakimbizi limekuwa mwiba katika ubavu wa siasa za UlayaPicha: picture-alliance/ZUMAPRESS.com

Seehofer ambaye ni mkuu wa chama cha Christian Social Union (CSU) cha jimboni Bavaria, ambacho ni mshirika mkuu wa chama cha Christian Democratic Union (CDU) cha Kansela Merkel, amesema  serikali iko njiani kuondoa kero zinazokipa umaarufu chama cha AfD, ambacho uchunguzi wa maoni wa hivi karibuni imeonyesha kwamba kinazidi kujiongezea wafuasi.

Wiki iliyopita msimamo mkali wa Horst Seehofer ulitishia kuisambaratisha serikali ya mseto wa vyama inayoongozwa na Kansela Merkel, hususan baada ya kutishia kujiuzulu ikiwa matakwa yake ya kuwafukuza mpakani wahamiaji waliosajiliwa katika nchi nyingine, yangeendelea kupuuzwa na Kansela Merkel.

Wiki hii vyama vitatu vinavounda serikali hiyo vilipata makubaliano ya kuharakisha mchakato wa kuwafukuza wahamiaji waingiao Ujerumani kutoka nchi nyingine za Ulaya, kwa kuheshimu sheria zilizopo katika Umoja wa Ulaya.

Mwandishi: Daniel Gakuba/dpae, ape

Mhariri: John Juma