Uchaguzi wa Septemba 24 machoni mwa walimwengu
8 Agosti 2017Mnamo wiki na miezi inayokuja, macho ya walimwengu yatazidi kukodolewa Ujerumani kuliko wakati wowote ule mwengine. Wengi wanafanya hivyo kwasababu wanavutiwa na kuithamini nchi hii. Lakini sio wote: Katika wakati ambapo baadhi wanashangaa na kujiuliza Ujerumani inawezaje kufanikiwa licha ya changamoto na matatizo, wengine wanahofia nchi hiyo isije ikageuka tena kuwa dola lenye madaraka makubwa kabisa kati kati ya bara la Ulaya.
Baadhi wanaiangalia Ujerumani na kansela wake Angela Merkel kama ngome ya mwisho inayouzuwia Umoja wa ulaya usivunjike. Wengine wanaituhumu Ujerumani kutaka kulazimisha kwa nguvu masharti yake yafuatwe. Na sio kwa masilahi ya Ulaya bali kwa masilahi yake wenyewe: Kila kitu kwa ajili ya masilahi ya dola hilo linaloongoza katika kusafirisha bidhaa nchi za nje na lenye kuzusha maajabu ya kiuchumi.
Kokote kule ninakojikuta ulimwenguni, ninakutana na watu ambao utayarifu wa Ujerumani wa kuwapokea wakimbizi zaidi ya milioni moja wanautaja kuwa ni kitendo cha utu, ukarimu mkubwa, au ninakutana na watu waliokasirika, wake kwa waume wanaotutuhumu kuwapokea wakimbizi wengi kama hao na kwa namna hiyo kubeba jukumu la kutoweka desturi na mila za nchi za magharibi.
Wajerumani wateremka vituoni Septemba 24 inayokuja
Kwa umuhimu sawa na huo ndivyo na sisi wajerumani tunavyozitilia maanani kampeni za uchaguzi mkuu unaokuja. Septemba 24 Ujerumani italichagua bunge jipya na kwa namna hiyo kuchagua nani ataiongoza siku za mbele nchi hii. Tukiwa Kituo cha Matangazo kwaajili ya nchi za nje, tunataka kuiitumia hali mpya ya uangalifu kuelezea kinachotokea nchini mwetu. Kinachowashughulisha wajerumani wanaoridhika moja kwa moja na mkondo unaofuatwa na serikali kuu iliyoko madarakani hivi sasa. Kinachowasumbua wale walioingiwa na hofu kuhusu maisha yao ya siku za mbele, kujikuta katika hali ya kutegemea au kuwalea watoto wao katika nchi ambayo machoni mwao hailingani tena na ile waliyokuwa wakiiangalia kuwa ni nchi yao. Eti kweli Ujerumani iko tayari kujitambulisha kuwa ni nchi ya uhamiaji? Au ushindi wa wafuasi wa siasa za kizalendo katika uchaguzi ni ushahidi kwamba wanasiasa wanafuata mkondo ambao raia, wake kwa waume hawakubaliani nao?
Tutafafanua pia ufanisi wa kiuchumi unasababishwa na nini, vipi unafanyakazi mfumo wa elimu nchini Ujerumani na kwa nini unatajikana kuwa mfumo wa aina pekee. Tutatoa wasifu wa wanasiasa wetu mashuhuri na bila ya shaka tutafafanua maajabu ya Angela Merkel anaegombea mhula wa nne, mwanasiasa mashuhuri kabisa ulimwenguni.
Utapata ufafanuzi wa sera za ndani na aje za Ujerumani
Na tutarajie nini kutoka kwa nani? Mkondo gani wa siasa ya nje? Majukumu ya muungano yana umuhimu wa aina gani? Jumuia ya kujihami ya NATO? Sera za maendeleo zina umuhimu gani? Au kuzidishwa gharama za kijeshi ndizo zinazomfanya mgombea awe muhimu? Jukumu la aina gani Ujerumani inapaswa kuwa nalo katika Umoja wa Ulaya?
Lakini katika safari yetu na utafiti tunataka pia kubadilishana maoni pamoja na nyie, wasomaji, watazamaji na wasikilizaji wetu. Maripota wetu watawauliza watu masuala kupitia # ask DW, katika maeneo yao na kuwaachia watoe maoni yao-.Tunakuombeni mchangie.Tunakuulizeni kile mnachotaka kukijua, kile tunachopaswa kukielezea na tunakuombeni mtupatie maoni yenu na tathmini yenu. DW tunataka mnamo miezi inayokuja tufungue jukwaa litakalowaruhusu walimwengu kujadiliana kwa lugha 30 kuhusu Ujerumani.
Mjadala miongoni mwa wana DW ulimwenguni
Na jukumu la aina gani Ujerumani inapaswa kuwa nalo siku za mbele, katika sekta ya usalama, ndani ya jumuia ya kjiham ya NATO na ndani ya Umoja wa ulaya. Mnatarajia nini kutoka serikali mpya? Kipi kinakutieni wasi wasi, nguvu na udhaifu wa Ujerumani zinakutokana wapi? Ripoti zetu mtazipata kupitia Hashtag "GermanyDecides" kupitia Twitter ,sawa na facebook,Tv na bila ya shaka katika mitandao yetu ya internet.
Tunafurahi kupokea michango yenu itakayochochea majadiliano. Na kwa msaada wa mtandao wa maripota wetu katika kila pembe ya dunia na idara zetu mijini Berlin na Bonn, tutafafanua kinachoendelea nchini Ujerumani na kwanini uchaguzi unaitishwa humu nchini September 24 inayokuja.
Mwandishi: Ines Pohl/Hamidou Oummilkheir
Mhariri: Mohammed Khelef