1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump athibitisha kifo cha kiongozi wa "Dola la Kiislamu"

27 Oktoba 2019

Rais wa Marekani Donald Trump amethibitisha kuwa vikosi maalum vya Marekani vimemuua kiongozi wa kundi linalojiita Dola la Kiislamu – IS Abu Bakr al-Baghdadi kaskazini mwa Syria

https://p.dw.com/p/3S1lO
Trump verkündet Tod von IS-Anführer Al-Bagdadi
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Harnik

"Jana usiku, Marekani ilifikisha mwisho safari ya gaidi nambari moja duniani," alisema Trump. "Al-Baghdadi amefariki dunia"

"Alifika mwisho wa handaki wakati mbwa wetu wakimfukuza,” Aliongeza Trump. Al-Baghdadi aliripua mabomu aliyokuwa amejifunga mwilini wakati wanajeshi walipomkaribia. Mlipuko huo uliwauwa wanawe watatu.

Vikosi maalum vya Marekani viliweza kumtambua Baghdadi dakika 15 baada ya kuuawa kwa kufanya vipimo vya vinasaba – DNA katika eneo la shambulizi hilo. Uchunguzi huo wa DNA ulikuwa muhimu ikizingatiwa kuwa al-Baghdadi alikuwa ametangazwa kuuawa mara kadhaa. Hakukuwa na hasara yoyote kwa upande wa Marekani wakati wa operesheni hiyo.

Zerstörung in Syrien
Kijiji cha Barisha, mkoa wa Idlib alikouawa al-BghdadiPicha: picture-alliance/AP Photo/G. Alsayed

Trump amesema katika Ikulu ya White House kuwa "idadi kubwa ya wapiganaji wa al-Baghdadi na marafiki waliuawa, wakati watoto 11 wadogo wakihamishwa kutoka kwenye nyumba walimokuwa, bila kujeruhiwa.

Amesema dunia sasa ni mahala salama, na kuwa "matukio hayo ni ukumbusho mwingine kuwa tutaendelea kuwawinda magaidi waliobaki wa IS hadi mwisho.”

Trump ameipongeza Urusi, Uturuki, Syria na Iraq klwa ushirikiano wao. Wizara ya Ulinzi ya Uturuki imesema katika taarifa kuwa Uturuki na Marekani zilibadilishana taarifa kuhusu shambulizi hilo lililoongozwa na Marekani mkoani Idlib, Syria. Kamanda wa vikosi vya Syrian Democratic – SDF, Mazloum Abdi ameandika kwenye Twitter kuwa kifo cha al-Baghdadi kilikuwa matokeo ya ushirikiano wao na Marekani.

Kwa miezi mitano kumekuwa na ushirikiano wa pamoja wa taarifa za kijasusi na uchunguzi mahsusi, hadi tulipofanikisha operesheni ya pamoja ya kumuua Abu Bakr al-Baghdadi,” Aliandika Abdi.

Al-Baghdadi amekuwa mafichoni mwa miaka mitano. Kuna wakati Marekani ilitangaza zawadi ya dola milioni 25 kwa yeyote ambaye alikuwa na taarifa ambazo zingesaidia kupatikana kwake.

Mnamo Aprili, al-Baghdadi alijitokeza kwenye video, ya kwanza tangu nyingine iliyotolewa 2014, siku chache baada ya kundi hilo kutangaza "ukhalifa” nchini Iraq na Syria.

Kwa miaka mingi, kulikuwa na madai kadhaa ya kifo cha al-Baghdadi ambazo baadaye zilithibitishwa kuwa za uwongo.