1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tetemeko la ardhi lawaua takriban watu 400 Indonesia

Caro Robi
29 Septemba 2018

Karibu watu 400 wamefariki dunia katika tetemeko kubwa la ardhi Indonesia huku hospitali zikijitahidi kuwashughulikia majeruhi na maafisa wa uokozi wakifanya operesheni za kuwaokoa waliokwama kisiwani Sulawesi.

https://p.dw.com/p/35hJt
Erdbeben Tsunami in Indonesien Palu
Picha: Getty Images/AFP/M. Rifki

Shirika la kitaifa la kukabiliana na mikasa na majanga limesema watu 384 wameuawa na tetemeko hilo, karibu wote kutoka mji wa Palu, lakini limeonya kuwa idadi ya waathiriwa inatarajiwa kuongezeka.

Mji wa Palu una wakazi karibu 350,000 na shirika la kukabiliana na mikasa na majanga la Indonesia limesema mamia ya watu waliokuwa wakijiandaa kwa tamasha iliyopaswa kufanyika katika fukwe za kisiwa hicho siku ya Ijumaa hawajulikani waliko.

Mamia wamejeruhiwa

Hospitali zimefurika watu waliopata majera, wengi wao wakitibiwa nje ya hospitali kutokana na kwamba hospitali haziwezi kuwapokea wagonjwa zaidi.

Indonesien Nach dem Erdbeben und dem Tsunami in Palu, Central Sulawesi
Majeruhi wakiwa wamelala nje ya HospitaliPicha: Getty Images/AFP/M. Rifki

Tsunami hiyo iliyokikumba kisiwa hicho cha Sulawesi, ilitokana na tetemeko kubwa la ardhi lililoyaporomosha majengo kadhaa mjini Palu na kusababisha wakaazi wa mji huo kukimbilia nyanda za juu.

Barabara hazipitiki, uwanja wa ndege wa Palu umefungwa kwa kipindi cha saa 24 zijazo na huduma za umeme, pia zimekatika kutokana na athari ya tetemeko hilo la ukubwa wa 7.5 kulingana na vipimo vya Ritcher.

Rais wa Indonesia Joko Widodo amesema jeshi limeagizwa kwenda katika eneo la mkasa kusaidia maafisa wa ukozi kupata majeruhi na kupata miili ya waliofariki.

Indonesia ni mojawapo ya nchi  zinazokumbwa na majanga ya kimazingira ya mara kwa mara duniani. Mapema mwaka huu, tetemeko kubwa la ardhi lilikikumba kisiwa cha Lombok na kisiwa jirani cha Sumatra na kuwaua watu 550.

 Mnamo mwaka 2004 tetemeko jingine la ardhi liliwaua watu 168,000 nchini humo. Mnamo mwaka 2010, karibu watu 430 waliuawa wakati tetemeko la ardhi lilipokunmba eneo la pwani la Sumatra na wengine 600 waliuawa katika kisiwa cha Java.

Mwandishi: Caro Robi/afp/Reuters/dpa

Mhariri: Zainab Aziz-Mtullya