1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania: Wananchi walalamika kukosa bidhaa muhimu

18 Januari 2022

Nchini Tanzania kumekuwa na kilio kikubwa cha wananchi kutokana na kuadimika na kupanda bei kwa baadhi ya bidhaa muhimu. Miongoni mwa bidhaa hizo ni vinywaji kama vile soda.

https://p.dw.com/p/45hbS
Tanzania - Plastikbeutel auf dem Markt
Picha: Getty Images/AFP/S. Khalfan

Hadi sasa bado haijafahamika sababu ya kuadimika kwa baadhi ya bidhaa hizo za vinywaji na hakuna taarifa yoyote iliyotolewa na waztengenezaji wake wala wasambazaji jumla.

Maeneo mengi ya masoko yaani maduka ya rejareja na yale makubwa yamekuwa yakishuhudiwa kuwa na aina fulani ya soda pekee huku baadhi ya aina nyingine za soda zikikosekana kabisa.

Manung'uniko ni mengi na wananchi wanasema, kama hali hiyo itaendelea kuachwa jinsi ilivyo basi kuna uwezekano mkubwa bei ya bidhaa hizo zikapanda maradufu. 

Kwa ujumla kilio hicho kinaonekana kutawala karibu maeneo yote ya nchi ambako taarifa zinasema maduka mengi yanakabiliwa na upungufu wa bidhaa hizo.

Tansania Markt Bananen Verkauf
Bidhaa ya ndizi ikiwa sokoni mjini ShinyangaPicha: DW/V. Natalis

Hata hivyo, ingawa baadhi ya taarifa kuonyesha kuwepo kwa maeneo kiasi ambayo yanaanza kushuhudia kurejea taratibu kwa huduma hizo, lakini watumiaji wengi bado wamepigwa na butwaa. 

Kutokana na ukubwa wa tatizo hilo, serikali imeanza kuingilia kati na tayari waziri wa uwekezaji, viwanda na biashara, Ashatu Kijaji ameagiza tume ya ushindani kuingilia kati na ameipa muda wa siku tatu kuja na majibu kwa nini hali hiyo imejitokeza wakati huu.

Mbali na kuadimika kwa bidhaa hizo za vinywaji vya soda, bei ya vifaa vya ujenzi inatajwa kuwa juu na inavyoonekana tatizo hilo la kupanda kwa bei ni la muda mrefu.