1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano unaongazia suala la rasilimali watu waanza Tanzania

26 Julai 2023

Wakuu wa nchi za Afrika wameanza mkutano unaongazia suala la rasilimali watu nchini Tanzania huku Rais Samia Suluhu Hassan akionya juu ya uwekezano wa bara hilo kuzalisha vijana watakaokosa matumaini kuhusu bara lao.

https://p.dw.com/p/4UPE9
Rais wa Tanzania - Samia Suluhu Hassan
Rais wa Tanzania - Samia Suluhu HassanPicha: Ericky Boniphace/AP/picture alliance

Rais Samia aliyefungua mkutano huo katika jiji kuu la kibiashara Dar es salaam amewatahadharisha viongozi wenzake juu ya haja ya kuchukua hatua madhubiti ili kuwasaidia vijana ambao idadi yao inazidi kuongezeka.

Amesema Afrika haiwezi kubaki salama kama mipango na vipaumbele vyake havitaakisi kukwamua changamoto na mahitaji yanayowakabili vijana ambao baadhi yao anasema wamelazimika kutorokea katika nchi za ng'ambo kwa matumaini kustawisha maisha yao.

Viongozi wa Afrika kuwa na ajenda moja kuhusu kuwastawisha vijana

Kiongozi huyo amesisitiza haja ya viongozi wa Afrika kuwa na ajenda moja inayozungumza kuhusu kuwastawisha vijana hasa katika wakati huu ambako dunia inaingia katika mapinduzi ya nne ya viwanda. Uendelezwaji vijana kwa njia ya kuwapatia mitaji, ujuzi pamoja elimu yenye ufanisi ni baadhi ya mambo yaliyowatawala katika hotuba yake iliyofungua mkutano huo ulianza jana kwa ngazi ya mawaziri. Rais Samia anataka viongozi wenye udhubutu wa kuwapigania na kuwajali vijana ili kuijenga Afrika yenye uchumi endelevu.

Afrika yalaumiwa kwa namna inavyoshindwa kuzitumia rasilimali zake

Vijana wahudhuria mkutano wa kisiasa mjini Kisumu nchini Kenya
Vijana wahudhuria mkutano wa kisiasa mjini Kisumu nchini KenyaPicha: Brian Ongoro/AFP

Mkutano huo umekuwa na nia ya kuongeza uwekezaji katika eneo la rasilimali watu ili kuongeza tija ya uzalishaji na makundi ya vijana ndiyo yanayotupiwa macho. Afrika ambayo wakazi wake wengi ni vijana wanaochukua asilimia 60 ya idadi jumla, imekuwa ikutupiwa lamawa kwa namna inavyoshindwa kuzitumia vyema rasilimali zake. 

Benki ya Dunia inataka mabadiliko katika mifumo ya sera

Benki ya Dunia iliyoshirikiana na Tanzania kuandaa mkutano huo, inataka mabadiliko katika mifumo ya sera ili kuharakisha mageuzi ya kiuchumi. Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, Dr Victoria kwakwa anasema Afrika inapaswa kuanza kukimbia kuelekea kwenye uchumi wa kimaendeleo ili kukabiliana na kundi kubwa la vijana lililoko nyuma yake. Ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana pamoja na ifunyu fursa za kimaendeleo kunatazamwa na wengi kuwa ni sawa na bomu linalosubiri kulipuka. Baadhi ya vijana hao wanasema viongizi wa Afrika wanapaswa kutembea katika maeneo yao.

Mkutano huo ukakahotikishwa leo jioni kwa tamko la pamoja Dar es salaam, unafanyika kwa mara ya kwanza barani Afrika na Tanzania ikiwa mwenyeji.