1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania: Kiwango cha uhuru wa wanahabari kimeshuka

Hawa Bihoga22 Agosti 2018

Kwa mujibu wa Baraza la habari Tanzania, waandishi wa habari wanahofia kuingia matatani dhidi ya serikali, hatua inayodhoofisha muhimili wa kupata taarifa kwa umma na imefanya kiwango cha uhuru wa wanahabari kushuka.

https://p.dw.com/p/33bD2
Kajubi Mukajanga
Picha: DW/E. Boniphace

Baraza la habari nchini Tanzania MCT, limesema kuwa hivi sasa kiwango cha uhuru wa wanahabari nchini humo kimeshuka kuliko kawaida, na hii ni kutokana na waandishi wa habari kuhofia kuingia matatani dhidi ya serikali hatua ambayo inadhoofisha muhimili wa kupata taarifa kwa umma. hayo yamesemwa na katibu mtendaji wa baraza hilo Kajubi Mukajanga na kuongeza kuwa, wanahababri, wahahriri na wamiliki wa vyombo vya hababri wanapitia vitisho, wakati wakitekeleza majukumu yao.

Inatajwa kuwa nguvu ya taaluma ya habari nchini inazidi kuporomoka kutokana na kile kinachotajwa kuwa, wanahabari wanahofia kuandika habari ambazo zitaudhi mamlaka, hatua ambayo inatafsiriwa kuwa inazidi kudhoofisha uhuru wa vyombo vya hababri nchini humo.

Akizungumza na DW katibu mtendaji wa baraza la habari nchini Tanzania MCT Kajubi Mukajanga amesema kuwa, kwa kipindi hiki wanahabari pamoja na wahariri wanajizuia kuandika baadhi ya mambo ili kutoiudhi mamlaka zilizopo, na hata kujitolea adhabu bila kuwepo kwa mlalamika wa juu ya taarifa inayowafanya kujiadhibu.

Ujumbe kwenye picha: Tunahitaji uhuru wa habari
Ujumbe kwenye picha: Tunahitaji uhuru wa habariPicha: DW/A. Juma

Wamiliki wa vyombo vya habari waingiwa hofu

Kajubi anaongeza kuwa hii haijaishia kwa wanahabari na wahahriri pekee, sasa imekwenda mbali zaidi hata kwa wamiliki wa vyombo vya habari kupata maonyo mbalimbali, hatua inayosababisha nao kupata hofu juu ya uwekezaji katika sekta ya habari.

Wakati haya yakishuhudiwa Tanzania imesaini mikataba mbalimbali ya kimataifa inayowalazimu kuzingatia haki za binadamu ikiwemo, uhuru wa kupata taarifa, lakini pia katiba ya nchi hiyo ibara ya kumi na nane inaonesha wazi juu ya haki ya kupata taarifa,hili linatajwa kuwa, mikataba hiyo imesalia katika makaratasi na kumalizwa nguvu na sheria za ndani ambazo zinatoa uhalali wa haya yanayoshuhudiwa kuendelea kutendeka.

lakini wanahababri wenyewe wanasema kuwa, haya yanaendelea kushuhudiwa kwa kuwa mamlaka zimeamua kuhalalisha sheria ambazo zinakandamiza uhuru wa utendaji kazi wa wanahabari na vyombo vya habari.

Wadau wa masuala ya habari wanasema kuwa, nguvu ya wanahabari inatosha katika kukabiliana na kile walichokiita dhuluma dhidi ya uhuru wa habari nchini humo, na hakuna muhimili mwingine ambao utakuja kuingilia kati na kuwaondoa katika hilo.

 

Mhariri: Josephat Charo