1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

''Sisi ni taifa ambalo lilivunja mipango ya adui'' Zelensky

Saleh Mwanamilongo
3 Machi 2022

Mashambulio ya makombora ya Urusi yameua raia 34 kwenye mkoa wa Kharkiv. Huku zaidi ya watu milioni moja wameikimbia Ukraine kufuatia uvamizi wa Urusi.

https://p.dw.com/p/47wHg
Mlipuko wakumba Kyiv huku Urusi ikiendeleza mashambulizi
Mlipuko wakumba Kyiv huku Urusi ikiendeleza mashambuliziPicha: Alisa Yakubovych/EPA-EFE

Gavana wa mkoa wa mashariki unaodhibitiwa na Ukraine wa Donetsk amesema mji wa bandari wa Mariupol, mmoja ya miji yaliolengwa na uvamizi wa Urusi,hauna huduma ya umeme na maji.

Kwa upande wake idara ya huduma za dharura ya Ukraine imesema raia 34 wameuliwa na makombora ya Urusi kwenyre mkoa wa Kharkiv mnamo masaa 24 yaliyopita.

Shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa, limesema leo alhamisdi kwamba zaidi ya watu milioni moja wameikimbia Ukraine toka kuanza kwa mashambulizi ya Urusi wiki moja iliopita.

Wanajeshi wa Urusi walionekana leo katikati ya bandari ya Ukraine ya Kherson, siku moja baada ya madai yanayokinzana kuhusu iwapo Moscow ililiteka eneo lolote muhimu nchini Ukraine toka uvamizi wake.

Wakati huohuo,wajumbe kutoka Urusi na Ukraine wanatarajiwa kufanya mazungumzo nchini Belarus,ikiwa ni duru ya pili ya majadiliano ya ana kwa ana tangu kuanza kwa mashambulizi ya Urusi.

Soma pia →UNHCR: Katika wiki moja, wakimbizi milioni waliikimbia Ukraine

''Mipango ya ujanja, ilioyajaa chuki kwa nchi yetu''

Rais wa Ukraine ametoa ujumbe mpya wa video kwa raia wake  akiwataka kuendelea na mapambano dhidi ya wavamizi wa Urusi
Rais wa Ukraine ametoa ujumbe mpya wa video kwa raia wake akiwataka kuendelea na mapambano dhidi ya wavamizi wa UrusiPicha: Ukraine Presidency press service/AFP

Katika hotuba ya video kwa taifa mapema leo Alhamisi, Rais wa Ukraine,Volodymyr Zelenskyy alitoa wito kwa raia wa Ukraine kuendelea na upinzani, lakini hakutoa maoni juu ya kama wanajeshi wa urusi wameuteka mji wowote.

''Sisi ni taifa ambalo lilivunja mipango ya adui katika wiki moja. Mipango iliyoandikwa kwa miaka mingi: ya ujanja, iliyojaa chuki kwa nchi yetu,na watu wetu.",alisema Zelensky.

Kauli yake imejiri baada ya Urusi kukubali kwa mara ya kwanza kwamba takriban askari wake 500 waliuawa katika mapigano hayo na karibu 1,600 kujeruhiwa. Ukraine bado kutoa takwimu kama hiyo ya majeruhi kwa vikosi vyake vya jeshi.

Soma pia→Umoja wa Mataifa waitaka Urusi kuondoka Ukraine

Ufaransa yawataka raia wake kuondoka Urusi

Idara ya huduma za dharura chini Ukraine imesema zaidi ya raia 2,000 wamekufa, ingawa haikuwezekana kuthibitisha madai hayo. Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imesema imerekodi vifo vya watu 136 raia, ikiwa ni pamoja na watoto 13, tangu kuanza kwa uvamizi mnamo Februari 24.

Leo Alhmisi, wanariadha wa Urusi na Belarus, wamepigwa marufuku kushiriki katika Michezo ya Olimpiki ya Walemavu ya Majira ya baridi ya Beijing kutokana na vita vya Ukraine. Na Ufaransa imewataka raia wake kuondoka nchini Urusi ikiwa uwepo wao huko sio muhimu.