1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Shinikizo lazidi kuongezeka kwa viongozi wa mapinduzi Niger

6 Agosti 2023

Shinikizo linazidi kuongezeka kwa viongozi wa mapinduzi ya kijeshi wa Niger wakati muda waliopewa na Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi - ECOWAS wa kumwachia rais Mohamed Bazoum unakaribia kumalizika leo

https://p.dw.com/p/4Up3U
General Abdourahmane Tiani
Picha: REUTERS

Ufaransa ambayo iliwahi kuitawala Niger enzi za ukoloni imesema itaunga mkono hatua yoyote itakayochukuliwa na jumuiya hiyo. Waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa Catherine Colonna baada ya kufanya mazungumzo na waziri mkuu wa Niger Ouhoumoudou Mahamadou amesema kuwa hatima ya Niger, utulivu wa taifa hilo na kanda nzima viko hatarini.

Soma pia: Watawala wa kijeshi Niger waomba msaada wa kundi la Wagner la Urusi

Hivi karibuni, Wakuu wa ulinzi wa nchi za Afrika magharibi za jumuiya ya ECOWAS walisema wamekamilisha mpango wa uwezekano wa kuingilia kati kijeshi nchini Niger.

Wamefikia uamuzi huo baada ya wasuluhishi wa nchi za ECOWAS kukataliwa kuingia katika mji mkuu wa Niger, Niamey au kukutana na kiongozi wa watawala wa kijeshi, Jenerali Abdourahmane Tchiani.