1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika: Serikali zadhoofisha mashirika ya haki za binadamu

21 Oktoba 2020

Shirika la haki za binadamu la Amnesty International limesema serikali za Afrika zinadhoofisha mashirika ya haki za binadamu kwa kushindwa kufuata maamuzi yake na kuyanyima rasilimali kwa ajili ya operesheni zake.

https://p.dw.com/p/3kDka
Tansania African Court of Human and people's Rights
Picha: DW/N. Natalis

Katika toleo la pili la ripoti ya Hali ya Mashirika ya Kikanda na Mifumo ya Haki za Binadamu ya Afrika 2019-2020, iliyotolewa katika siku ya maadhimisho ya Haki za Binadamu Afrika, Amnesty International imesema mifumo iliyowekwa ya kulinda haki za binadamu barani kote inkabiliwa na changamoto kubwa, na alau moja unakabiliwa kitisho cha kuwepo.

Ripoti hiyo inaonya kwamba mustakabali wa Mahakama ya Haki za binadamu na Haki za Watu ya Afrika uko mashakani kufuatia uamuzi wa serikali za mataifa matatu - Benin, Cote d'Ivoire na Tanzania, kuondoa haki ya mtu mmoja mmoja na mashirika yasiyo ya kiserikali kufugua kesi katika mahakama hiyo. Rwanda iliondoa haki hii mwaka 2016 na kufanya jumla ya mataifa yaliozuwia njia ya kupata haki kuwa manne.

Soma pia:Amnesty International yamtaka rais Tshisekedi kutekeleza ahadi yake 

Amnesty International imegundua kuwa Benin, Cote d'Ivoire na Tanzania ziliondoa haki katika kujibu maamuzi waliyoyachukulia kuwa yasiowapendeza, na katikati mwa kuongezeka kwa hali ya kukosa uvumilivu kwa watetezi wa haki na kuporomoka kwa hali ya haki za binadamu kitaifa.

Amnesty International Protest Wahlen in Malin 2013
Shirika la Amnesty International limethibitisha kuwa serikali za Afrika zinaendelea kudhoofisha mashirika ya haki za binadamu.Picha: picture-alliance/dpa/W. Kumm

Tanzania iliondoa haki hiyo Novemba 2019, ikidai kwa upotoshaji kwamba mahakama hiyo ilikubali kushughulikia masuala ambayo yalipaswa kushughulikiwa na mahakama za kitaifa. Benin na Cote d'Ivoire zilijiondoa Machi na Aprili 2020 mtawalia.

Tanzania kuwasilisha ripoti ya haki za binaadamu, UN

Benin ilitofautiana na amri ya mahakama hiyo kusitisha ukamataji wa mali za mlalamikaji katika mzozo wa benki, ikidadi amri hiyo inadhoofisha maslahi ya kiuchumi ya taifa na utulivu wa kisiasa.

Soma pia: Amnesty imeilaumu Ulaya kwa mateso ya wahamiaji Libya

Cote d'Ivore ilikasirishwa na uamuzi wa mahakama kusitisha waranti wa kimataifa wa kukamatwa kwa waziri mkuu wa zamani Guillaume Soro, na kuwaachia kwa dhamana wanasiasa 19 wa upinzani, ikidai kwamba mahakama hiyo iliingilia mamlaka yake ya ndani.

Amnesty  inasema uamuzi wa mataifa hayo kuishambulia mahakama kwa uamuzi wake wasiokubaliana nao ulikuwa wa kutia wasiwasi.

Linasema mataifa ya Afrika yanapaswa kujizuwia kutumia nguvu za kisiasa dhidi ya taasisi ambazo lengo lake ni kuhakikisha haki inapatikana kwa kila mmoja, bila kujali siasa za serikali zao.

Soma pia: Amnesty International lafunga virago India

Tanzania yaongoza kwa kesi nyingi

Tansania African Court of Human and people's Rights
Mwandishi wa DW Veronica Natalis akizungumza na rais wa mahakama ya haki za binadamu na haki za watu Afrika, Jaji Slyvan Ore.Picha: DW/N. Natalis

Hadi sasa mahakama ya Afrika ya haki za binadamu imetoa hukumu nyingi zaidi dhidi ya Tanzania. Nchi hiyo pia ina idadi kubwa ya kesi zinazosubiri dhidi yake, ambapo nyingi zinahusu haki katika mchakato wa mashtaka.

Burkina Faso ndiyo nchi pekee ambayo imefuata kikamilifu hukumu za mahaka ya Afrika. Tanzania imetii kwa sehemu na Cote d'Ivoire imewasilisha ripoti ya utekelezaji kwa mahakama hiyo.

Benin, Kenya, Libya na Rwanda ambazo hukumu zimetolewa dhidi yake, hazitatekeleza maagizo ya mahakama hiyo hata kidogo, baadhi zikitangaza kwa ufedhuli kwamba hazitotii maagizo na hukumu za mahakama hiyo.

Soma pia: Amnesty International: Wakimbizi wa ndani nchini Somalia wakabiliwa na dhiki kubwa

Shirika la Amnesty International linasema serikali pia zimepuuza haki za watu wenye ulemavu na wazee kwa kushindwa kuridhia mikataba inayohusiana na ulinzi wa makundi hayo.  Amnesty imebaini kuwa hakuna hata nchi mwanachama mmoja ya Umoja wa Afrika iliyoridhia mkataba kuhusu watu wenye ulemavu barani Afrika, miaka miwili tangu mkataba huo ulipopitishwa.

Vile vile, miaka mitano tangu mkataba kuhusu watu wenye ulemavu kupitishwa Januari 2016, ni mataifa mawili tu ya Benin na Lesotho yaliouridhia.

Chanzo: Amnesty International