1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sensa Tanzania: Asilimia 93 wahesabiwa

Babu Abdalla Florence Majani
29 Agosti 2022

Kamishna Mkuu wa sensa ya watu na makaazi 2022 Anne Makinda amesema asilimia 93.45 ya kaya zote Tanzania zimehesabiwa kufikia leo Jumatatu Agosti 29, 2022.

https://p.dw.com/p/4GAjv
Tansania Dar Es Salaam | Kariakoo Markt | Händler
Picha: Said Khamis/DW

Zoezi la ukusanyaji takwimu za watu na makazi nchini Tanzania linakamilika usiku leo Agosti 29 huku kiwango cha  kaya zilizohesabiwa ni asilimia 93.4  na kaya asilimia 6.65 zikiwa bado hazijahesahibiwa.

Kutokana na idadi hiyo ya asilimia sita ya kaya ambazo hazijahesabiwa, Kamishna wa sensa Anne Makinda, amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa makarani wa sensa ili kuhakikisha zoezi hilo linakamilika leo wakati zoezi hilo linahitimishwa.

Kamishna huyo amesema kwa wananchi ambao hawajahesanbiwa, watatakiwa kwenda ofisi za serikali za mitaa, kuacha namba ya simu ili makarani wafike pale alipo mwananchi na taarifa zake sikusanywe.

Bi. Makinda amesema bado wapo makarani wa kutosha kwa ajili ya kuhakikisha zoezi hilo linakamilika hasa kwa maeneo yenye uhitaji, kadhalika amesema ofisi ya taifa ya takwimu, imeandaa namba maalum ambayo itakwenda moja kwa moja makao makuu Dodoma, ili makarani wafike kule ambako kaya hazijafikiwa na zoezi hilo.

Baadhi ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam, wametoa maoni yao kuhusu zoezi hilo na baadhi wamesema zoezi hilo lilikwenda vyema na baadhi wamesema hawajaelewa kwa nini taarifa zao zimechukuliwa.

Zoezi hilo kwa mwaka huu, limegubikwa na changamoto kadhaa ikiwamo vifaa vya kiteknolojia vilivyotumika kukusanya takwimu maarufu kama vishkwambi, kwisha chaji, kuibiwa, baadhi ya maeneo kutofikika kwa sababu ya miundombinu duni na kukosa mitandao.

Sensa ya Watu na Makazi ni zoezi la kitaifa linalofanyika kila baada ya miaka 10 ambapo Sensa ya mwisho kufanyika nchini ni ile ya mwaka 2012.

Hivyo Sensa ya mwaka 2022 itakuwa ni sensa ya Sita kufanyika nchini baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.

Sensa nyingine zilifanyika mwaka 1967, 1978, 1988, 2002 na 2012.