1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Scholz asema shambulizi la kisu Solingen ni ´ugaidi´

26 Agosti 2024

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz ameliita shambulizi la kisu la wiki iliyopita kuwa ni "ugaidi dhidi ya kila mmoja" na kuahidi mabadiliko na kuahidi hatua za haraka za kuimarisha udhibiti wa silaha.

https://p.dw.com/p/4jwKO
Ujerumani Solingen | Olaf Scholz
Kansela Olaf Scholz wa Ujerumani alipotembelea eneo la shambulio la kisu huko Solingen.Picha: Ina Fassbender/AFP/Getty Images

Scholz amesema kwenye mkutano na waandishi wa habari mjini Solingen kwamba shambulizi hilo lilikuwa ni la kigaidi na lililotishia jinsi watu wanavyoishi kwa umoja.

Scholz aliyeambatana na maafisa waandamizi wa kisiasa alisisitiza kuanzisha hatua za kuimarisha sheria za silaha na hasa matumizi ya visu, na kuahidi kufanya liwezekanalo kuhakikisha wale wasioweza kuishi Ujerumani, wanarejeshwa.

"Tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba wale wote ambao hawawezi kuishi hapa Ujerumani wanarejeshwa makwao kwa kutumia kanuni za kisheria ambazo tumekubaliana hivi karibuni."

Shambulizi hilo limezusha mjadala kuhusu uhamiaji nchini Ujerumani. Mtuhumiwa wa shambulizi hilo, raia wa Syria alijisalimisha Jumamosi jioni na kukiri, baada ya kujificha kwa siku nzima.