1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Scholz akiri matokeo ushindi wa AfD unatia wasiwasi

2 Septemba 2024

Chama cha AfD kimepata matokeo yake mazuri zaidi kwenye uchaguzi katika majimbo mawili ya Mashariki mwa Ujerumani, kikishinda jimboni Thuringia na kushika nafasi ya pili katika jimbo la Saxony.

https://p.dw.com/p/4kCKN

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz ameyaita matokeo ya uchaguzi katika majimbo mawili yaliyokipatia ushindi mkubwa chama cha mrengo mkali wa kulia cha AfD kuwa yanayoumiza, huku akivitaka vyama vikuu kuunda serikali bila ya vyama vyenye misimamo mikali ya mrengo wa kulia.

Chama cha Mbadala wa Ujerumani ama AfD kimekuwa cha kwanza cha mrengo mkali wa kulia kushinda uchaguzi wa jimbo nchini Ujerumani tangu Vita vya Pili vya Dunia, kufuatia ushindi kwenye jimbo la Thuringia jana Jumapili. Kwenye jimbo la Saxony chama hicho kimeshika nafasi ya pili.

Ujerumani | Uchaguzi wa jimbo Thuringia 2024 | Höcke
Mgombea mkuu wa AfD jimboni Thuringia Bjorn Hoeck alitangazwa kuwa fashisti.Picha: Chris Emil Janflen/IMAGO

Soma pia: Scholz akiri matokeo yaliyokipa ushindi chama cha AfD yanatia wasiwasi

Scholz aliyezungumza kama mbunge wa chama chake cha Social Democrats, SPD, ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba matokeo ya AfD huko Saxony na Thuringia yanatia wasiwasi na kulionya taifa kuwa hilo haliwezi kukubalika, akisema chama AfD inaivuruga nchi, kudidimiza uchumi, kuigawa jamii na kuharibu sifa ya Ujerumani.  

Hata hivyo, AfD kinachotajwa na idara ya usalama wa taifa nchini Ujerumani kama cha mrengo mkali wa kulia, bado hakiwezi kuunda serikali kwa kuwa vyama vingine hadi sasa vimekataa kushirikiana nacho.