1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

RSF:Ujerumani imeporomoka kwa uhuru wa habari

3 Mei 2022

Ripoti mpya ya Waandishi wa Habari Wasio na Mipaka kwa siku ya Uhuru wa Vyombo ya Habari Duniani inaonesha Ujerumani imeporomoka kwa uhuru wa habari kwa nukta tatu ikilinganishwa na mwaka uliopita

https://p.dw.com/p/4AlLA
Frankreich Paris | Bericht zur Pressefreit - Reporter ohne Grenzen
Picha: PHILIPPE LOPEZ/AFP/Getty Images

Taifa hilo limeshika nafasi ya 16 katika jumla ya 180 ikiwa nyuma ya mataifa kama Lithuenia, Jamaica na Ushelisheli. Hali katika ukanda wa Afrika mashariki imeonekana kuboreka kwa kiwango fulani. 

Shirika hilo la waandishi wa habari wasio na mipaka limetaja sababu tatu za kuporomoka kwa uhuru wa habari kwa Ujerumani kuwa ni sheria ambazo zinawaweka hatarini waandishi na vyanzo vyao, kupungua kwa hali ya vyombo vya habari kusikika kwa umma na juu ya yote vurugu katika nyakati za maandamno nchini humo.

Kwa mujibu wa shirika hilo ambalo liliweza pia lilibaini rekodi mbaya kwa Ujerumani kwa mwaka uliopita na ambapo kulibainika visa 65, imethibitisha visa vipya 80 dhidi ya waandishi, ikiwa ni idadi kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa tangu shirika hilo lianze kazi hiyo mwaka 2013. Idadi kubwa ya mashambulizi yalifanywa katika kipindi cha maandamano, hii ikiwa na maana matukio 52 kati ya 80 hayo yametokea katika kipindi hicho. Hii inatajwa kutokea katika kipindi cha maandamano ya kupinga masharti ya kukabiliana na kusambaa kwa virusi vya corona.

Afrika Mashariki hali imenawiri kwa kiasi.

Nixon Kichinda, Station Manager, ATG Radio
Nixon Kichinda wa ATG Radio ya NairobiPicha: Stephen Mutonji

Kwa ukanda wa Afrika Mashariki Kenya imewekwa katika nafasi ya 69 ambayo ni bora ikilinganishwa na mwaka jana ilipokuwa katika nafasi ya 102, Burundi iko katika nafasi ya 107 kutoka ya 147 mwaka jana, inafuatia na Tanzania iliyosonga mbele nafasi moja kutoka 124 mwaka jana hadi 123 mwaka huu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imejikuta katika nafasi ya 124 kutoka 147 ya mwaka jana, Uganda ni nchi pekee ya ukanda huo iliyopiga hatua nyuma, ikiwa katika nfasi ya 132 mwaka huu ikilinganishwa na 125 ya mwaka jana, na Rwanda iko nafasi ya mwisho Afrika Mashariki ikiwekwa katika nafasi ya 136, ambayo lakini ni bora zaidi ya mwaka jana ilipikuwa katika nafasi ya 156.

Kwengineko Afrika hali imezidi kuwa mbaya zaidi katika mataifa kama Cameroon, Guinea Bissau, Mali na kwengineko baada ya mapinduzi hali ya vyombo vya habari imezidi kuwa tete haua ambayo inawafanya waandishi kuzingatia hali ya usalama wao kuliko yale muhimu ya kitaifa.

Soma zaidi:RSF: Idadi ya juu zaidi ya wanahabari walikamatwa mwaka 2021

Kambodscha Ministerpräsident Hun Sen
Shirika la utangazaji la Ufaransa RFI, lilifungiwa nchini Mali kutokana na kutangaza habari zilizouchukiza utawala nchini humo.Picha: AFP/Getty Images

Mapema mwezi Machi mamlaka ya udhibiti wa vyombo vya habari ya Mali ilitangaza kuwa kusitisha shughuli za shirika la utangazaji la Ufaransa (RFI) na France 24 kwa kile kilicholezwa vituo hivyo kutangaza taarifa iliyotaja vitendo vya ukiukwaji wa haki za binaadamu ambavyo vinafanya na jeshi la Mali kwa ushirikiano wapiganaji mamluki wa Urusi nchini humo.

Wakati Rais wa Zambia Hakainde Hichilema alishinda uchaguzi wa Agosti 2021 nchini humo, alitangaza mara moja kwamba atapanua wigo wa uhuru wa vyombo vya habari. Angewapa waandishi wa habari fursa  hata a kumfika yeye kwa urahisi, maafisa wengine wa serikali na taasisi, na kuanzisha mswaada wenye kuiboresha sekta hiyo. Hata hivyo hadi sasa bado kumekuwa na lawama za uhuru wa habari huku, Mwandishi mmoja wa michezo Emily Lukwesa akisema ni mapema mno kufanya tathimni kwa uhuru wa habari kwa taifa hilo.

Ripoti hii ya Jumanne inayataja mataifa matatu bora zaidi kwa uhuru wa vyombo vya habari kuwa ni Norway, Denmark na Sweden. Lakini nchi 10 ambazo hali yake ni mbaya zaidi duniani ni pamoja na Myanmar ya 176, ambapo mapinduzi ya Februari 2021 yalirudisha uhuru wa vyombo vya habari kwa miaka 10, pamoja na China, Turkmenistan 177, Iran 178, Eritrea 179 na Korea Kaskazini 180.

Vyanzo/ DPA/DW