1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya SIPRI: Matumizi ya kijeshi yaongezeka duniani kote

24 Aprili 2023

Mfumuko wa bei,vita vya nchini Ukraine na mvutano baina ya China na Marekani ni masuala yanayosababisha manunuzi ya silaha ya kiwango cha kuvunja rekodi. Nchi nyingi zilinunua silaha kwa kiwango kikubwa mnamo mwaka 2022.

https://p.dw.com/p/4QTLi
Finnland - Ukraine I Finnische Reservisten des Guard Jaeger Regiments
Picha: Alessandro Rampazzo/AFP

Ripoti ya kila mwaka ya taasisi ya kimataifa ya utafiti wa masuala ya amani ya mjini Stockholm, SIPRI, inasema bajeti za kijeshi ziliongozeka kwa asilimia 3.7 mnamo mwaka 2022 kulinganisha na manunuzi ya mwaka uliotangulia. Mtaalamu aliyeshiriki katika kuandika ripoti hiyo Nan Tian ameiambia DW kwamba nchi ziliongeza manunuzi ya silaha bila ya kujali hali ya kiuchumi ni mbaya au nzuri. Baada ya Urusi kuivamia Ukraine nchi nyingi za Ulaya zimekuwa zinaongeza bajeti zao za kijeshi.

Kutoka kushoto: Sigrn Rawet, Naibu Mkurugenzi, Jan Eliasson, Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi ya SIPRI, Princess Victoria na Dan Smith Mkurugenzi SIPRI.
Kutoka kushoto: Sigrn Rawet, Naibu Mkurugenzi, Jan Eliasson, Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi ya SIPRI, Princess Victoria na Dan Smith Mkurugenzi SIPRI.Picha: TT/imago images

Katika nchi za mfungamano wa kijeshi wa NATO, bajeti za kijeshi zilianza kuongezeka mnamo mwaka 2014 baada ya Urusi kukiteka kisiwa cha Ukraine cha Crimea sambamba na kuwaunga mkono waliojitenga mashariki mwa Ukraine. Nchi wanachama wa NATO zimeamua kuongeza matumizi ya kijeshi kwa asilimia 2 hadi mwaka ujao.

Tazama:

Licha ya manunuzi ya silaha kufikia Euro trilioni 2 duniani kote kiasi hicho kinawakilisha asilimia 0.1 ya pato jumla. Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita India, China na Israel zimekuwa zinaongeza bajeti zao za kijeshi. Katika kipindi hicho China iliongeza bajeti ya ulinzi kwa asilimia 63, India kwa asilimia 47 na Israel kwa asilimia 26. Hata hivyo mfumuko wa bei umesababisha kupungua kwa bajeti za kijeshi kulinganisha na uwiano wa tija ya kiuchumi. Uwezo wa kununua umepungua kutokana na kupanda kwa  bei za bidhaa za mahitaji ya kila siku.

Soma:Ripoti: Ukraine yawa muagizaji wa tatu wa silaha duniani, 2022

Kuongezeka kwa bei ya maziwa maana yake pia ni kuongezeka kwa bei ya ndege za kivita. Ripoti ya taasisi ya utafiti wa masuala ya amani ,SIPRI inabainisha hali hiyo. Kupanda kwa gharama za maisha pia ni tatizo kubwa nchini Ujerumani. Kutokana na vita vya nchini Ukraine jeshi  la Ujerumani limetengewa Euro bilioni 100 zaidi katika bajeti yake.

Kifaru cha jeshi la Ujerumani aina ya Leopard 2
Kifaru cha jeshi la Ujerumani aina ya Leopard 2Picha: U.S. Army/ABACA/picture alliance

Matumizi ya kijeshi, si kununua silaha tu.Kuongezeka kwa matumizi kunajumuisha pia kutoa msaada wa kijeshi kwa nchi nyingine ambao umefikia kiwango kikubwa kutokana na vita vya nchini Ukraine. Kulingana na utafiti Marekani pekee imeshatoa msaada wa dola bilioni 47 kwa Ukraine.

Soma:Ripoti ya SIPRI: vita vya nchini Ukraine vyasababisha ongezeko katika mahitaji ya silaha

Mnamo mwaka uliopita Marekani ilitumia dola bilioni 877 kwa ajili ya ulinzi. Kiasi hicho kinawakilisha asilimia 39 ya bajeti ya kijeshi ya dunia nzima. China inashika nafasi ya pili kwa matumizi ya dola bilioni 292. Wataalamu wa masuala ya kijeshi pamoja na wanasiasa wa Marekani wanatahadharisha kwamba China inaziba pengo la kijeshi kati yake na Marekani. Hata hivyo nchi hizo zinalenga shabaha tofauti za kijeshi.