1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa UAE amtangaza mwanawe kuwa mrithi wa kiti cha ufalme

30 Machi 2023

Kiongozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan amemteuwa mwanawe Sheikh Khaled kuwa mrithi wa Ufalme wa Abu Dhabi, mji mkuu wa taifa hilo la Ghuba wenye utajiri wa mafuta.

https://p.dw.com/p/4PUgU
 Sheikh Khaled bin Mohamed bin Zayed Al Nahyan
Picha: Ryan Carter / Crown Prince Court/Abu Dhabi/AP/picture alliance

Aidha amewateuwa kaka zake kushika nyadhifa nyingine kuu serikalini. Sheikh Mohammed, ambaye alichukua usukani kama rais na mtawala wa Abu Dhabi mwaka jana, amemtangaza kaka yake Sheikh Mansour kuwa makamu wa rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, pamoja na mtawala wa Dubai Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum.

Hatua hiyo yumkini inaongeza nguvu za mamlaka ya dola hiyo kwenye mji wa Abu Dhabi, ambao ni kiti cha kisiasa kwa kuzingatia utajiri wake mkubwa wa mafuta.

Sheikh Mohammed amewateuwa kaka zake wengine Sheikh Tahnoun bin Zayed Al Nahyan, ambaye ni mshauri wa usalama wa taifa wa Umoja wa Falme za Kiarabu anayedhibiti himaya hiyo kubwa ya kibiashara, na Hazza bin Zayed Al Nahyan kuwa manaibu watawala wa Abu Dhabi.