1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Samia: Tanzania haiwezi kujengwa na chama kimoja

Deo Kaji Makomba
5 Aprili 2022

Rais Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Tanzania haitajengwa na chama kimoja na kwamba ni lazima kuwe na ushirikiano. Rais Samia ametoa kauli hiyo wakati akifungua mkutano wa kitaifa wa haki, aamani na maridhiano.

https://p.dw.com/p/49Tf8
Tansania Präsidentin  Samia Suluhu Hassan
Picha: Eric Boniphase/DW

Akizungumza katika mkutano huo ulioshirikisha baadhi ya vyama vya siasa na wadau wa maendeleo na washiriki katika shughuli za kisiasa kutoka ndani na nje, Rais Samia amesema Tanzania haitajengwa na chama kimoja au mtu mmoja na kwamba watanzania wote wanapaswa kushirikiana kuijenga nchi hiyo katika misingi iliyo sawa.

Kadhalika Rais Samia amesema hakuna atayesaidia katika kutafuta haki isipokuwa watanzania wenyewe huku akiwataka washiriki katika mkutano huo kuzungumza haki katika mazingira ya kitanzania.

Chadema Chairman Freeman Mbowe
Mwenyekiti wa Chadema Freeman MbowePicha: Ericky Boniphace/DW

Rais  Samia amezungumzia suala la vyama vya siasa huku akisema vinao umuhimu mkubwa katika kuangalia na kukosoa yale yanayoendelea katika serikali na kutoa maoni yao ili kuirekebisha serikali iliyoko madarakani huku akisisitiza kuwa serikali yake itaendelea kushirikiana na vyama vya siasa.

Hata hivyo wakati Rais Samia akifungua mkutano huo wa kitaifa wa haki, amani na maridhiano baadhi ya vyama vya siasa nchini Tanzaniavimesusia mkutano huo huku vikisema kuwa kutaniko hilo ni kama danganya toto na kwamba hauna masilahi mapana kwa taifa la Tanzania.

Mkutano huo wa haki, amani na maridhiano unafanyika jijini Dodoma huku ukishirikisha vyama vya siasa, wadau wa maendeleo huku vyama vingine vya siasa vikisusa kwa kile kinachoelezwa hauna masilahi mapana kwa taifa la Tanzania. CHADEMA na NCCR-Mageuzi ni miongoni mwa vyama vilivyosusia mkutano huo.