1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raia nchini Rwanda kusalia nyumbani kwa wiki nzima

Sylvanus Karemera19 Januari 2021

Serikali ya Rwanda imetangaza zuio la kukaa ndani kwa muda wa wiki kwa wakazi wote wa mji mkuu wa nchi hiyo kutokana na kupanda kwa idadi ya maambukizi ya virus vya corona. 

https://p.dw.com/p/3o6wV
Afrika | Motorradfahrer mit einem Trikot der deutschen Fußball-Nationalmannschaft in Ruanda
Picha: picture-alliance/dpa/imageBROKER

Uamuzi huu umekuja siku moja baada ya serikali kutangaza uamuzi mwingine wa kuzifunga shule zote za awali, za msingi na sekondari mjini Kigali kwa sababu hiyo hiyo ya ongezeko la virus vya corona. Baraza la mawaziri lililoongozwa na Rais wa Rwanda Paul Kagame ndilo limetangaza hatua hiyo.

Waziri afya wa Rwanda Dr Daniel Ngamije amesema kwamba mji mkuu wa Rwanda Kigali unakabiliwa na hatari kubwa ya maambukizi kutokana na idadi ya watu wanaopoteza maisha yao kila siku kutokana na virus vya janaga la corona.

"Tunapofanya tathmini tunaona kwamba mnamo siku 50 zilizopita kuanzia sasa unaonyesha kwamba idadi ya watu zaidi ya elfu 11 walioambukia tangu kilipotokea kisa cha kwanza mwaka jana,asilimia 46% ya watu hao wamepatikana ndani ya kipindi hicho.Lakini pia asilimia 65% ya watu 142 waliokwishapoteza maisha yao nao wamekufa ndani ya siku 50 zilizopita na wengi wako mjini Kigali, hii ikiwa na maana kwamba siku hizi 50 zilizopita mambo yameharibika", amesema Ngamije.

Rwanda Kigali | Beatmungsgeräte | Manufaktur in Kigali
Mashine ya kupumua iliyotengenezwa nchini RwandaPicha: DW/S. Karemera

Wananchi wametangaza hali ya wasiwasi kutokana na baadhi yao kuhisi uwezekano wa kupoteza fursa za kazi na mahitaji mengine.

Agizo la baraza la mawaziri limeagiza sehemu zote za huduma kufungwa na hakuna anayeruhusiwa kutoka nje isipokuwa kwa sababu za msingi bila hata hivyo kupata idhini ya polisi. Msemaji wa polisi Kamishina wa polisi John Bosco Kabera ameonya yeyote atakayekwenda kinyume na haya.

Shule zafungwa mjini Kigali kutokana na COVID-19

"Sisi hatupendi kuona tukimkamata mtu lakini tukilazimika tufanya hivyo kwa hiyo tunawaomba watu mjini Kigali kusalia nyumbani".

Huku hayo yakijiri, Taasisi ya Tiba nchini Rwanda, RBC imearifu kuwa imepata vifaa vya kisasa vya kuweza kutunza aina zote za chanjo, zikiwemo zile zinazohitaji kuhifadhiwa katika ubaridi wa nyuzi zaidi ya 80 za sentigredi chini ya sufuri. Bado haijabainika lini dozi za chanjo zitawasili nchini Rwanda.