1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaEthiopia

Mfanyabiashara haramu ya binaadamu akamatwa

6 Januari 2023

Shirika la Polisi la Kimataifa, Interpol limesema raia wa Eritrea ambaye anatajwa kuwa mmoja wa watu wanaofanya biashara haramu ya kusafirisha binadamu wanaosakwa zaidi duniani, amekamatwa nchini Sudan.

https://p.dw.com/p/4LoBg
Logo Interpol
Picha: EPA/WALLACE WOON/dpa/picture alliance

Interpol ilisema jana kuwa mtu huyo aliyetambulika kama Zekarias Habtemariam, anatuhumiwa kwa kuongoza genge la uhalifu ambalo linawateka watu nyara, kuwanyang'anya mali zao na kuwaua wahamiaji wa Afrika Mashariki wanaojaribu kuvuka Bahari ya Mediterania kutoka Libya.

Habtemariam alikamatwa siku ya Jumapili katika oparesheni kubwa iliyofanywa na polisi wa kimataifa, ikiongozwa na Umoja wa Falme za Kiarabu, UAE.

Kwa mujibu wa Interpol, Waziri wa Mambo ya Ndani wa UAE, Saeed Abdullah al-Suwaidi, amesema operesheni hiyo ilidumu kwa miezi tisa na iliwahusisha polisi wa Uholanzi, Ethiopia na Sudan.

Awali, Habtemariam alitoroka akiwa chini ya ulinzi nchini Ethiopia, wakati akikabiliwa na mashtaka ya biashara ya magendo mwaka 2020.