1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa wataka Narges Mohammad aachiwe huru

6 Oktoba 2023

Wakati pongezi, kutoka pande tofauti za ulimwengu zikitolewa kwa mshindi wa Tuzo ya Nobel, Narges Mohammadi, Umoja wa Mataifa umetaka kuachiliwa huru kwa mtetezi huyo wa haki za wanawake.

https://p.dw.com/p/4XDZV
Friedensnobelpreisträgerin 2023 l  Narges Mohammadi l Zuschnitt NEU Cinemascope
Picha: Mohammadi family archive photos/Handout via REUTERS

Msemaji wa ofisi ya Haki za Binadamu ndani ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva, Liz Throssell amesema wanawake wa Iran wamekuwa chanzo cha msukumo kwa ulimwengu, wamekuwa na ujasiri na azimio katika sura ya matukio ya ukandamizaji.

Ameongeza kwa kusema watatoa miito ya kuachiliwa huru na kuachiwa huru kwa watetezi wote wa haki za binaadamu walio gerezani nchini Iran. Msemaji wa Umoja wa Mataifa Alessandra Vellucci amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres "amekuwa wazi sana katika utetezi wa haki za wanawake na wasichana nchini Iran."

Ufaransa, Ujerumani zatoa pongezi

Kama ilivyofanya Ufaransa, serikali ya Ujerumani nayo imesema imeupokea vyema uamuzi wa kumtaja mwanaharakati wa haki za wanawake wa Iran aliye gerezani, Narges Mohammadi kuwa mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mwaka huu wa 2023. Akizungumza kutoka mjini Berlin, naibu msemaji wa serikali ya Ujerumani, Christiane Hoffmann amesema tuzo ya Bi Narges ni kiwakilishi cha wanawake wote jasiri wa Iran wanaosimama kidete katika kutetea usawa wa haki za binadamu.

Ehemann von Narges Mohammadi | Gewinnerin Friedensnobelpreis 2023
Mume wa Nargis Muhammad, Taghi Rahman akionesha picha ya familia yake.Picha: Thibault Camus/AP Photo/picture alliance

Zaidi anasema "Serikali ya Ujerumani imefurahi kwamba Narges Mohammadi ametunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mwaka huu na inampongeza kwa moyo mkunjufu kwa tuzo hii. Tuzo la Bibi Nargees pia inawakilisha wanawake wote jasiri wa Iran ambao wanasimamia usawa na haki za binadamu, mara nyingi katika vihatarishi vya maisha na uhuru wao.”

Nargis atoa kauli kutoka gerezani baada ya kupata tuzo

Mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel ambae pia ni Muiran,Shirin Ebadi amesema anamatumani kuwa tuzo ya mwaka huu iliyokwenda kwa Narges Mohammadi itafanikisha demokrasia na usawa kwa wanawake wa Irani.

Pamoja na kutoa pongezi kwa mshindi huyo amesema tuzo hiyo itaweka wazi ukiukwaji wa haki za wanawake nchini Iran, ambao kwa bahati mbaya serikali imeonesha kutokuwa tayari kuubadilisha.

Aidha mshindi huyo, Narges mwenyewe amezungumza na gazeti la New York Times na kusema uungwaji mkono wa dunia na kutambulika kwa jitihada zake za utetezi wa haki za binaadamu kunamfanya awe mwenye kuwajibika zaidi, mwenye moyo mkunjufu na mwenye matumaini zaidi.

Urusi yajizuia kusema lolote kuhusu Tuzo ya Nobel

Kwa uoande wake Ikulu ya Urusi-Kremlin, mshirika wa Iran imekataa kusema loloze kuhusu uamuzi wa Kamati ya Tuzo ya Nobel, kumpa ushindi Narges. Msemaji wa Ikulu hiyo Dmitry Peskov amewaambia waandishi wa habari "Hapana, hatuna cha kusema," pale alipotakwa afanye hivyo na waandishi hao.

Soma zaidiIran inakabiliwa na rekodi mbaya ya haki za binaadamu na ukiukwaji wa haki za wanawake

Kwa mujibu wa mume wake,Taghi Rahmani, kutoka na kifungo chake katika gereza la Evin, mjini Tehrain Narges hajaweza kuwaona watoto wake kwa muda wa miaka saba sasa na yeye mwenyewe kama mume miaka 15. Kwa mujibu wa tovuti ya Tuzo ya Amani ya Nobel, mwanaharakati huyo amekamatwa na mamlaka ya Iran mara 13 na kuhukumiwa jumla ya miaka 31 gerezani kulikoambatana na adhabu ya viboko 154.