1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nigeria yateua kamanda mpya kupambana na Boko Haram

Yusra Buwayhid
11 Novemba 2018

Nigeria imeteua kamanda mpya wa kuongoza operesheni ya kupambana na kundi la Boko Haram, ukiwa ni uteuzi wa tano wa aina hiyo katika kipindi cha chini ya miaka miwili.

https://p.dw.com/p/382oB
Nigeria Soldaten in Damboa
Picha: Getty Images/AFP/S. Heunis

 Nigeria imemteua kamanda wake wa tano wa jeshi katika kipindi cha miaka miwili kuongoza vita dhidi ya ugaidi wa kundi la Boko Haram, kulingana na taarifa za Jumamosi za jeshi la nchi hiyo. Kulingana na duru za kijeshi hatua hiyo imechukuliwa kutokana na kuendelea kwa mashambulizi ya kundi hilo.

Mashambulizi hayo yanaweza kuhatarisha uwezekano wa Muhammadu Buhari kuchaguliwa tena kama rais wa nchi hiyo katika uchaguzi ujao wa mwezi Febuari. Wakati wa kampeni za uchaguzi uliopita, Buhari aliahidi kukomesha uasi wa kundi la Boko Haram lakini mashambulizi ya kundi hilo pamoja na kundi dogo lilojigawa linalojiita Dola la Kiislam la Afrika Magharibi (ISWA) yanaingia mwaka wake wa 10.

Nafasi ya Jenerali Mkuu Abba Dikko aliyechukua wadhifa huo wa mwezi Julai kuiongoza operesheni iliyopewa jina la Lafiya Dole, itapokewa na Jenerali Mkuu Benson Akinroluyo, kama ilivyoeleza taariga ya jeshi la Nigeria.

Dikko amehamishiwa katika Idara ya Jeshi ya Masuala ya Kiraia kujaza nafasi ya mkuu wa masuala ya kijeshi.

Mashambulizi ya Boko Haram yameongezeka

Nigerianische Rebellen Niger Delta
Mwanamgambo wa Boko HaramPicha: picture-alliance/AP Photo/G. Osodi

Maafisa wawili waliozungumza bila ya kutaja majina yao, wamesema jenerali huyo amehamishwa kazi kutokanana na kuongezeka kwa mashambulizi ya Boko Haram tokea achukue nafasi hiyo.

Tokea Julai, wakati Dikko alipoteuliwa, wanajeshi kadhaa wa Nigeria wameuawa katika mapambano na wanamgambo, na kundi la ISWA limewaua wafanyakazi wawili wa kutoa misaada ya kibinadamu baada ya kuwateka.

Wanajeshi pia walifanya maandamano katika uwanja wa ndege mwezi Septemba. Msemaji wa jeshi hakujibu ujumbe mfupi wa maneno kwa njia ya simu wala simu alizopigiwa kutaka atoe maelezo zaidi juu ya uamuzi huo wa kumuondoa Dikko kama kamanda wa vita dhidi ya wanamgambo wa siasa kali za kidini, miezi michache baada ya kupewa cheo hicho.

Mwandishi: Yusra Buwayhid/rtre

Mhariri: Bruce Amani