1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

New York: Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, ...

29 Novemba 2003
https://p.dw.com/p/CFwj
ameripoti kwamba Israel imeshindwa kuambatana na takwa la Hadhara Kuu ya Umoja wa Mataifa kwamba iwache kujenga ule unaoitwa Ukuta wa Usalama katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. Hadhara Kuu ya Umoja wa Mataifa iliunga mkono mwezi uliopita kwa kura 144, nne zikipinga, na nchi 12 hazijashiriki, azimio lililoitaka Israel iwache kuujenga ukuta huo. Mwakilishi wa Palastina, Nasser al-Kidwa, amesema atataka kiitishwe kikao cha dharura cha hadhara hiyo wiki ijayo ili kupitisha azimio la pili litakaloitaka Mahakama ya Kimataifa kutoa hukumu kama ukuta huo sio halali. Ukuta huo umepangwa kuwa na urefu wa kilomita 500 kutoka kaskazini hadi kusini mwa Ukingo wa wa Magharibi wa Mto Jordan.
<br><br>
Kwa upande mwengine, mazungumzo yasiokuwa rasmi ya siku mbili mjini London baina ya wa-Israeli na Wapalastina kuhusu mwenendo wa amani yamemalizika. Pande zote mbili zilisema mazungumzo hayo yalifanyika katika hali nzuri, lakini hakujapatikana maelewano kuhusu mpango wa ramani ya amani ya Mashariki ya Kati. Katika mazungumzo hayo walishiriki mshauri wa usalama wa kiongozi wa Wapalastina, Yasser Arafat, na mtoto wa kiume wa waziri mkuu wa Israel, Ariel Sharon. Rais Arafat alitoa mwito katika barua aliyowaandikia wakuu wa nchi kadhaa za Magharibi akiwataka wajitahidi kuuanzisha tena mwenendo wa amani.