1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Aminata Toure aweka historia katika siasa za Ujerumani.

8 Julai 2022

Toure aliweka historia alipoapishwa kama waziri katika jimbo la kaskazini mwa Ujerumani la Schleswig-Holstein wiki iliyopita na kuwa Mwafrika wa kwanza mwenye uraia wa Ujerumani kuketi katika bunge la jimbo hilo.

https://p.dw.com/p/4DqME
Deutschland, Kiel | Aminata Touré nach der Vereidigung als Ministerin
Picha: Marcus Brandt/dpa/picture alliance

Binti wa wakimbizi wawili kutoka Mali, Aminata Toure sasa anaongoza Wizara ya Masuala ya Kijamii ya jimbo hilo.

Mwanasiasa huyo wa chama cha Kijani aliviambia vyombo vya habari vya Ujerumani kwamba aliona jukumu lake kama "maalum" kutokana na ujumbe mwingi aliopokea kutoka kwa watu waliomwambia kuwa kuteuliwa kwake kunamaanisha " mambo mengi kwao".

Msichana huyo mwenye umri wa miaka 29 amesema atachukua pia fursa hiyo kupigania usawa na kupinga itikadi kali za mrengo wa kulia.

Masuala hayo yamekuwa lengo lake tangu alipopigiwa kura kwa mara ya kwanza katika bunge la jimbo la Schleswig-Holstein mnamo mwaka 2017.

Sio mara ya kwanza kwa Toure kupata nafasi muhimu ya kisiasa. Mnamo mwaka wa 2019, alichaguliwa kama naibu spika wa bunge la jimbo na kuwa Mjerumani wa kwanza mwenye asili ya Afrika na mwanasiasa mdogo kushikilia wadhifa kama huo katika majimbo yote 16 ya Ujerumani.

Anajivunia kuwa Mjerumani mwenye asili ya Afrika

Toure alizaliwa mwaka wa 1992 huko Neumünster, mji wa viwanda na wenye ukubwa wa wastani kaskazini mwa Ujerumani, ambako wazazi wake walikuwa wakiishi baada ya kuondoka nchini Mali.

Alitumia miaka mitano ya kwanza ya maisha yake katika makazi ya wakimbizi na hatimaye alipata uraia wa Ujerumani alipokuwa na umri wa miaka 12.

Toure hutumia neno "Afro-German" kujitambulisha. Aliiambia DW katika mahojiano na idhaa ya Kifaransa mapema mwaka huu kuwa, kujitambulisha huko kunamuonyesha kama mtu mwenye asili ya Afrika lakini ambaye nyumbani kwake ni Ujerumani.

Vitisho kutoka kwa watu wasiyojulikana

Hofu ya familia yake kufukuzwa nchini Ujerumani ilichagiza uamuzi wake wa kuanza kujihusisha na siasa na alijiunga na chama cha Kijani mwaka 2012, mwaka huo huo alianza kusoma sayansi ya siasa na Kifaransa katika chuo kikuu nchini Ujerumani.

Toure alishinikiza kwa muda mrefu kuhusu mapokezi bora na ya haraka kwa wakimbizi nchini Ujerumani. Na msimamo huo ulimsababishia maadui kadhaa na kupelekea vitisho kutoka kwa watu wasiojulikana.

Lakini mwanasiasa huyo chipukizi katika siasa za Ujerumani anasema hataruhusu mambo hayo kumtisha.

Kabla ya kuapishwa kwake kuwa waziri, Toure aliviambia vyombo vya habari vya Ujerumani vya RND kuwa, nia yake ya kufanikiwa katika siasa iliimarishwa na wazazi wake, ambao hawakuchoka kumwambia kuwa, kama mtu wa kikundi cha walio wachache, angelazimika kujituma kwa asilimia 200 wakati wengine wakijituma kwa asilimia 100.

Uzoefu wake umeimarisha imani yake kwamba siasa za Ujerumani zinahitaji kuwa jumuishi zaidi. Amesema, sera zinapaswa pia kutolewa na watu wanaoelewa mtazamo wa wale ambao bado wana uwakilishi duni katika jamii.

Na ingawa "wasifu sio mbadala wa siasa." Hivi majuzi Toure aliiambia Dw kuwa maisha aliyoyapitia mtu "yana ushawishi juu ya jinsi maamuzi ya kisiasa huchukuliwa.

Haja ya utofauti zaidi katika siasa

Kama mtu ambaye amepitia vitendo ubaguzi wa rangi, lakini pia kuungwa mkono na watu wanaoamini umuhimu wa kazi yake, Toure anataka kuwa mfano kwa watu wengine kutoka makundi ya walio wachache.

" Sio rahisi kuwa mwanamke katika jamii, na mimi kuwa mwanamke katika nchi ambayo raia wengi ni wazungu, ilikuwa vigumu sana. Nilikabiliana na vitendo vya ubaguzi wa rangi katika nchi hii lakini pia nilipata uungwaji mkono. Inaweza kuwa rahisi kwa watu wengi kuingia katika siasa ikiwa tayari kuna mtu kama wao aliyewatangulia. Na ndio maana sitaki liwe jambo la nadra kwa mwanamke wa kiafrika kuwa katika siasa, nataka liwe jambo la kawaida."

Kama alivyoandika katika kitabu chake "We can be more: The power of diversity", anasema raia wa Ujerumani wanapaswa kujivunia wale wote waliochangia kuifanya nchi hiyo kuwa ya demokrasia na wale ambao bado wanapigania kuimarisha utawala wa sheria.

(DW)