1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwanamfalme Philipp ameaga Dunia

9 Aprili 2021

Ufalme wa Uingereza umepoteza moja ya rasilimali zake kubwa zaidi, Mume wa Malkia aliedumu kwa muda mrefu katika historia ya Uingereza.

https://p.dw.com/p/3rm0D
England I Prinz Philip I The Duke of Edinburgh
Picha: Matt Dunham/WPA/Getty Images

Kwa kifo cha Mwanamfalme Philipp ambaye ndiye mume wa Malkia aliedumu kwa muda mrefu katika historia ya Uingereza, ufalme wa Uingereza umepoteza mmoja ya rasilimali zake kubwa zaidi. Akiwa mwanafamilia mrefu zaidi wa ufalme nchini Uingereza, usingekosa kumuona Mwanamfalme Philip. Kwa kuwa ni mume wa Malkia, muda wake mwingi maishani, alilazimika kuwa kwenye kivuli cha Malikia Elizabeth wa Pili.  Maisha yake yalikuwaje?

Mara nyingi Mwanamfalme Philip ambaye pia ni mtawala wa Edinburgh, ametajwa kuwa mtu mwenye sifa za zamani, lakini pia alifahamika kwa mitindo iliyopitwa na wakati ya ucheshi usiofaa kisiasa, hali ambayo mara nyingine ilimfanya kuchekwa.

Alizaliwa mwaka 1921 kwa mwanamfalme Andrew wa Ugiriki na Denmark. Leo ni vigumu kutafakari kuhusu mizizi yake yenye utata na Ujerumani, alipomuoa mwanamfalme mdogo kule Westminister Abbey London mnamo mwaka 1947, mnamo wakati makovu ya Vita Vikuu vya Pili Duniani bado yalikuwa akilini mwa wengi nchini Uingereza.

Großbritannien London Queen feiert 90.Geburtstag mit Phillip
Picha: picture-alliance/PA Wire/Evening Standard/A. Lentati

Mapenzi

Lakini mapenzi yalikuwa ya dhati ya kifalme. Kwenye harusi yao, Mfalme George wa Sita alisema binti yetu anaolewa na mume anayempenda. soma zaidi Malkia Elizabeth II wa Uingereza atimiza miaka 92

Akiwa mvulana pekee na mtoto wa tano wa mwanamfalme Andrew wa Ugiriki na binti mfalme Alice wa Battenberg, Philip alikuwa na mizizi ya kifalme ya Kijerumani na Uholanzi katika hedikota iliyojulikana kama Schleswig-Holstein-Sonderburg-Glucksburg.

Alizaliwa katika mji wa Corfu wakati kukiwa na vita kati ya Ugiriki na Uturuki, na hivyo kuilazimisha familia yake kuenda mafichoni akiwa mchanga.

Alikutana na Elizabeth kwa mara ya kwanza alipokuwa na umri wa miaka 18. Wakati huo Elizabeth akiwa na umri wa miaka 13. Elizabeth aliambatana na baba yake Mfalme George wa Sita alipozuru chuo cha kijeshi ambako Philip alikuwa akijifunza. Wakaanza kuandikiana barua na baadaye mapenzi yakaota kati yao. Mnamo mwaka 1946, Philip alimuomba mfalme amruhusu amuoe bintiye na mfalme alikubali.

BG Prinz Philip Herzog Duke of Edinburgh | Elizabeth II. u Philipp beim Tanz 1947
Picha: akg-images/picture-alliance

Alichukua uraia wa Uingereza mwaka 1947 alipochukua jina la Kianglikana Mountbatten lililo kuwa na maana sawa na jina la familia ya mama yake.

Malkia Elizabeth wa Pili alipochukua usukani mwaka 1952,  itifaki ilimlazimu Mwanamfalme Philip atembee na Malkia kila mara, huku akiwa hatua chache nyuma yake.

Baadaye alionekana na wengi kama mhimili katika familia hiyo ya kifalme.

Baadhi ya wachambuzi wamehoji kwamba sifa yake ya kujieleza waziwazi ilikuwa njia moja ya kufidia jukumu lake la kuwa kama nguzo. Wengine pia husema sifa hiyo ya kujieleza kinaganaga ilikuwa jaribio lake la kupunguza mhemko, jambo ambalo halikufaulu kila mara.

Kwa miongo mingi amefanya ziara 637 kivyake nje ya nchi na kutoa takriban hotuba 5,500

Mwanamfalme Philip alistaafu kutoka kwenye nyadhifa za kifalme mwaka 2017 alipokuwa na umri wa miaka 96.

Großbritanien I Prinz Philip  The Duke of Edinburgh
Mwanamfalme PhillipPicha: Steve Parsons/PA Wire/dpa/picture alliance

Makosa na utani

Makosa yake ya mara kwa mara yaligonga vichwa vya habari na kulazimisha kasri la Buckingham kutoa taarifa za mara kwa mara kuomba radhi. Mfano mnamo mwaka 1997, alimuita aliyekuwa kansela wa Ujerumani kwa wakati huo Helmut Kohl ”Reichskanzler” ikiwa ni jina la cheo kilichokuwa kikitumiwa na Adolf Hitler.

Inadaiwa kuwa wakati mmoja alitishia kumtupa nje Malkia Elizabeth wa pili kupitia dirisha la gari kwa sababu malkia alilalamika kuhusu uendeshaji wake wa gari kwa kasi sana.

Inaripotiwa kwamba alipokuwa Australia, alikutana na jamaa aliyesema ”Mke wangu ni dokta wa falsafa na mengine mengi zaidi yangu” kisha Philip akajibu, Ah tuna hiyo shida pia katika familia yangu.

Mara kwa mara utani wake ulikuwa mkali. Mnamo mwaka 1963 alimwambia Dikteta wa Paraguay Alfredo Stroessner kwamba, ni furaha kuwa katika nchi ambayo haitawaliwi na raia wake.

Mnamo mwaka 1967 alipoulizwa kama angependa kuzuru Muungano wa Kisovieti, alijibu kwa kusema ”Naam ningependa sana kuenda Urusi japo hao wanaharamu waliua nusu ya familia yangu.”

Mizizi ya Ujerumani

Chimbuko lake lilimtongea pakubwa maishani. Mizizi yake ya Ujerumani ilisababisha wengi nchini Uingereza kusita kumuamini, licha kwamba alihudumu katika jeshi la majini la Uingereza wakati wa vita. Soma zaidi Malkia wa Uingereza kuwasilisha mpango wa serikali ya Theresa May bungeni

Mnamo mwaka 1956, alipotaka kuanzisha tuzo ya Mtawala wa Edinburgh iliyolenga kuwahamasisha vijana kujipa changamoto kimwili na kiakili ili kujijengea imani kupitia masuala ambayo ni tofauti na elimu, wazo hilo halikupokelewa vyema na waziri wa Elimu David Eccles. Accles alimwambia nimesikia kwamba unajaribu kuanzisha ‘Uhitler' kwa vijana.

 

Mwandishi: Wagener, Volker

Tafsiri: John Juma