1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwanafunzi auawa wakati upinzani Kenya ukifanya maandamano

21 Machi 2023

Mwanafunzi mmoja aliuawa nchini Kenya jana wakati makabiliano kati ya vikosi vya usalama na waandamanaji wanaoipinga serikali yalipamba moto.

https://p.dw.com/p/4OyCs
Kenia l Proteste in Nairobi l Ausschreitungen mit der Polizei
Picha: Brian Inganga/AP/picture alliance

Ni baada ya kiongozi mkongwe wa upinzani Raila Odinga kuitisha maandamano ya kila wiki kuhusu kupanda kwa gharama ya maisha.

Polisi wa kupambana na ghasia waliwafyatulia mabomu ya kutoa machozi na mizinga ya maji waandamanaji na msafara wa Odinga huku vurugu zikizuka kati ya waandamanaji waliowarushia mawe polisi katika maeneo ya mji mkuu Nairobi na kwingineko.

Soma pia: Maandamano yashuhudiwa Kenya na Afrika Kusini

Katika mji wa Maseno ambao ni ngome ya upinzani, magharibi mwa Kenya, polisi ilisema mwanafunzi wa chuo kikuu aliuawa baada ya maafisa kufyatua risasi za moto wakati wa vurugu na waandamanaji waliokuwa wakiwarushia mawe. Wanasiasa waandamizi ni miongoni mwa watu kadhaa waliokamatwa na kuwachiwa baadae.