1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mpinzani wa Kongo atangaza muungano na waasi

16 Desemba 2023

Mpinzani wa Kongo Corneille Nangaa anayeishi uhamishoni nchini Kenya, ametangaza kuundwa kwa muungano wa kisiasa na kijeshi na waasi wa M23 pamoja na makundi mengine yenye silaha

https://p.dw.com/p/4aF1E
Aliyekuwa mwenyekiti wa tume ya uchaguzi Kongo - Corneille Nangaa wakati wa mkutano na wanahabari katika makao makuu ya CENI mjini Kinshasa mnamo Desemba 20, 2018
Aliyekuwa mwenyekiti wa tume ya uchaguzi Kongo - Corneille NangaaPicha: Luis Tato/AFP

Tangazo la Nangaa limeisababisha serikali ya Kongo kuionya Kenya kuhusu kile ilichokiita "athari zinazoweza kujitokeza'' kwa kumruhusu Nangaa kuishi nchini humo. Nangaa, ambaye alikuwa mwenyekiti wa tume ya uchaguzi ya Kongo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2018, alitoa wito wa "muungano wa vikosi vyote vya kijeshi, kisiasa na kijamii" ili "kujenga upya serikali" na "kurejesha amani" katika taifa hilo linalokumbwa na mapigano.

Nangaa ameema vikundi tisa vimeungana naye

Nangaa ameongeza kuwa vikundi vipatavyo tisa vinavyojumuisha M23, tayari vimeungana naye kupitia muungano wake wa "Congo River Alliance" unaolenga kuleta kile alichokiita " Umoja na Utulivu wa kitaifa". Alitetea kuundwa kwa muungano huo kama jibu kwa kile alichokiita ''udhaifu wa serikali '' ya Kongo katika muda wa miongo mitatu na kushindwa kwake ''kudumisha mamlaka nchini kote.''

Msemaji wa serikali ya Kongo amesema kutakuwa na athari za kidiplomasia na Kongo

Msemaji wa serikali ya Kongo Patrick Muyaya, alitaka maelezo kutoka Kenya kwa kuwa mwenyeji wa kile alichosema ni ''shughuli za uasi'', na kuita tangazo hilo "kuwa la kukosa uzalendo" na pia kuongeza kuwa Nangaa anapaswa kuona aibu.

Muyaya amesema ni wazi kutakuwa na athari za kidiplomasia.