1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mlanguzi mkuu wa madawa ya kulevya Colombia akamatwa

24 Oktoba 2021

Mlanguzi mkuu wa madawa ya kulevya nchini Colombia "Otoniel" amekamatwa, wamesema maafisa kutoka nchini humo, wakiitaja hatua hii kama ushindi mkubwa kwa nchi ambayo ni muuzaji mkubwa wa cocaine duniani.

https://p.dw.com/p/4279I
Kolumbien Dairo Antonio Usaga bekannt als "Otoniel" festgenommen
Picha: Colombian presidential press office/AP/picture alliance

Dairo Antonio Usuga aliyekuwa mkuu wa kundi kubwa zaidi la ulanguzi wa dawa za kulevya nchini humo linaloitwa Gulf Clan, alikamatwa karibu na mojawapo ya kambi zake kuu mjini Necocli, karibu na mpaka wa Panama. Picha zilizotolewa na serikali zimemuonyesha "Otoniel" kama anavyoitwa kwa utani, mwenye umri wa miaka 50 akiwa amefungwa pingu na kuzungukwa na maafisa wa polisi.

Rais wa Colombia Ivan Duque, amefananisha kukamatwa kwa Dairo Antonio  Usuga na kukamatwa miongo mitatu iliyopita kwa aliyekuwa mlanguzi mkubwa Pablo Escobar.

"Hili ni pigo kubwa kwa ulanguzi wa dawa za kulevya nchini mwetu katika karne hii," alisema Rais Duque.

Kulala mvuani kwa hofu ya maafisa wa polisi

Mkuu wa polisi wa Colimbia, Jorge Vargas, katika kikao na waandishi wa habari amesema walifanya operesheni ya angani kwa kutumia setlaiti kwa ushirikiano na Marekani na Uingereza.

Kolumbien Drogenbaron Pablo Escobar
Mlanguzi wa zamani wa madawa ya kulevya Colombia Pablo EscobarPicha: Imago/Zuma Press

Waanajeshi 500 na ndege 22 aina ya helikopta zilitumwa katika manispaa ya Necocli kufanya operesheni hiyo ilyopelekea kifo cha mwanajeshi mmoja.

Kulingana na polisi, Otoniel alikuwa amejificha msituni katika eneo la Uraba ambako ndiko anakotokea na alikuwa hatumii simu ila alikuwa anategemea wajumbe kwa mawasiliano.

Kwa mujibu wa Vargas, kwa hofu ya maafisa wa polisi, Otoniel alikuwa akilala msituni huku akinyeshewa na mvua kwani alikuwa anaogopa kukaribia maeneo yanayokaliwa na watu.

Otoniel ambaye ni mbabe wa kivita, amekuwa mafichoni kwa zaidi ya mwongo mmoja na amekuwa akifanya hivyo kwa kuwahonga maafisa wa serikali na kujaribu kuwa na uhusiano mzuri na maafisa wa kijeshi.

Kundi la Gulf Clan, ambalo wanachama wake wametekeleza mauaji pakubwa na kuwahangaisha watu kaskazini mwa Colombia, limekuwa likipigania kuchukua udhibiti wa njia za kusafirisha cocaine kimagendo kupitia misitu ya kaskazini mwa nchi hiyo hadi Amerika ya Kati na kuingia Marekani.

Otoniel na kakake walianza kama wapiganaji

Kwa muda mrefu, mlanguzi wa madawa ya kulevya amekuwa akisakwa na Marekani na nchi hiyo ilikuwa imetoa kitita cha dola milioni 5 kwa yeyote atakayetoa taarifa zitakazopelekea kukamatwa kwake.

Kolumbien Drogenschmuggel 8 Tonnen Kokain beschlagnahmt
Tani za cocaine zilizokamatwa na polisi ya Colombia mwaka 2016Picha: picture-alliance/dpa/Colombian Police

Serikali ya Colombia inalilaumu kundi la Gulf Clan, linalofadhiliwa na fedha za ulanguzi wa dawa za kulevya, uchimbaji madini haramu na uhalifu, kwa matukio mabaya ya ukosefu wa amani kote nchini humo tangu mwaka 2016 ambapo serikali ilitia saini mkataba wa amani na waasi wa FARC.

Usuga na kakake ambaye alifariki mwaka 2012 kufuatia uvamizi wa mwaka 2012, walianza kama wapiganaji wa kundi la Popular Liberation Army mwaka 2012.

Mwaka 2017, sura ya Otoniel ilionekana kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, baada ya kuchapisha video wakati wa ziara ya kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis nchini humo, akitaka kundi lake likubaliwe kusalimisha silaha kama sehemu ya mpango wa amani.

Vyanzo: AP/AFPE