1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUrusi

Mkuu wa ujasusi Urusi asema matamshi ya Macron ni ya hatari

6 Machi 2024

Mkuu wa Shirika la Ujasusi la Urusi amesema matamshi ya rais Emmanuel Macron wa Ufaransa juu ya uwezekano wa kutumwa wanajeshi wa Jumuiya ya NATO nchini Ukraine yanatishia kuitumbukiza dunia kwenye vita vya nyuklia.

https://p.dw.com/p/4dCt9
Sergei Naryshkin
Mkuu wa Shirika la Ujasusi la Urusi, Sergei NaryshkinPicha: Sergei Fadeichev/TASS/dpa/picture alliance

Akizungumza kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni, jasusi huyo mkuu wa Urusi, Sergei Naryshkin, amesema matamshi ya Macron yanadhihirisha tabia ya viongozi barani Ulaya ya kupuuza masuala nyeti, akionya  matamshi ya aina hiyo ni ya hatari.

Wiki iliyopita, rais Macron alisema kuna uwezekano kwa mataifa barani Ulaya kutuma wanajeshi wake nchini Ukraine lakini akatahadharisha kuwa mwafaka wa pamoja kuhusu jambo hilo bado haujapatikana. 

Matamshi yake yalikosolewa na Urusi huku baadhi ya mataifa ya magharibi ikiwemo Marekani na Ujerumani yakijitenga na msimamo huo yakisema hayana mipango ya kutuma wanajeshi wake ndani ya ardhi ya Ukraine.