1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yasema vita dhidi ya Hamas vitaendelea

27 Desemba 2023

Mkuu wa jeshi la Israel, Luteni Jenerali Herzi Halevi, ameeleza kuwa vita vya kulimaliza kundi la Hamas vitaendelea kwa miezi kadhaa huku shinikizo la kimataifa la kusitisha mapigano likiongezeka.

https://p.dw.com/p/4ac7H
Nahostkonflikt | Bodenoffensive der israelischen Armee im Gazastreifen
Picha: IDF/Xinhua/picture alliance

Mkuu huyo wa jeshi la Israel amesema mapigano dhidi ya wanamgambo wa kundi la Hamas katika Ukanda wa Gaza wenye wakazi wengi yanafanyika katika mazingira yenye utata.

Mkuu wa jeshi la Israel Luteni Jenerali Herzi Halevi
Mkuu wa jeshi la Israel Luteni Jenerali Herzi Halevi alipowasili katika Kamandi ya Kusini kukutana na makamanda na askari wa akiba ili kuidhinisha mipango ya kuendelea kwa mapigano dhidi ya Hamas katika Ukanda wa Gaza, Jumatano Oktoba 11, 2023.Picha: IDF/UPI Photo/Newscom/picture alliance

Luteni Jenerali Herzi Halevi, amesema hayo huku jeshi la Israel likizidisha mashambulizi ndani ya Ukanda wa Gaza, ambapo mpaka sasa zaidi ya watu 20,000 wameripotiwa kuuawa.

Soma Pia:Hamas, Islamic Jihad wakataa pendekezo la Misri kuachia madaraka Gaza

Wakati huo huo maafisa wakuu wa Marekani wanakutana na waziri wa maswala ya mikakati wa Israel katika Ikulu ya Marekani huku kukiwa na shinikizo la kimataifa la kusitisha mapigano. Rais wa Marekani Joe Biden amejadili na Emir wa Qatar  SheikhTamim bin Hamad Al Thani juu ya kuachiliwa kwa mateka waliosalia ambao wanaoshikiliwa na kundi la Hamas wakiwemo raia wa Marekani.

Kushoto: Rais wa Marekani Joe Biden. Kulia: Emir wa Qatar Sheikh Tamim bin Hamad al-Thani.
Kushoto: Rais wa Marekani Joe Biden. Kulia: Emir wa Qatar Sheikh Tamim bin Hamad al-Thani.

Biden na bin Hamad al Thani walijadili pia juhudi zitakazowezesha kuongezeka kwa mtiririko wa misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza. Marekani, Umoja wa Ulaya na nchi kadhaa za magharibi zimeliorodhesha kundi la Hamas kama kundi la kigaidi.

Soma Pia:UN yamteua Sigrid Kaag kama mratibu mpya wa misaada Gaza

Wakati hayo yakiendelea Umoja wa Mataifa umemteua naibu waziri mkuu wa zamani wa Uholanzi Sigrid Kaag kuwa mratibu wake wa maswala ya kibinadamu wa Gaza.

Waziri mkuu wa zamani wa Uholanzi, Sigrid Kaag, mratibu mpya wa Umoja wa Mataifa atakayesimamia misaada kwa ajili ya Gaza.
Waziri mkuu wa zamani wa Uholanzi, Sigrid Kaag, mratibu mpya wa Umoja wa Mataifa atakayesimamia misaada kwa ajili ya Gaza.Picha: Sem Van Der Wal/ANP/dpa/picture alliance

Kaag ni mtaalam wa maswala ya Mashariki ya Kati na jukumu lake litakuwa ni kusimamia usafirishaji wa misaada ya kwenda Gaza kama sehemu ya Azimio la Baraza la Usalama lililopitishwa siku ya Ijumaa kwa lengo la kuongeza nguvu hatua za kupelekwa misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.

Vyanzo: AFP/DPA/DW