1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Misri, Ufaransa, Ujerumani na Jordan zaionya Israel

Deo Kaji Makomba
7 Julai 2020

Nchi za Misri, Ufaransa, Ujerumani na Jordan wameionya Israel Jumanne hii dhidi ya kunyakua sehemu ya mipaka ya Palestina, huku zikisema kuwa kwa kufanya hivyo kunaweza kuwa na athari kwa uhusiano wa nchi hizo mbili. 

https://p.dw.com/p/3ev1j
Symbolbild I Gaza I Nahost-Konflikt I Israel Luftwaffe I Golanhähe
Picha: Getty Images/AFP/J. Marey

Katika taarifa iliyosambazwa na Wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani, nchi hizo ambazo ni pamoja na washirika wawili wanaoongoza wa Israel katika mashariki ya kati, wamesema mawaziri wao wa mambo ya nje wamejadili jinsi ya kuanzisha mazungumzo kati ya Israel na Mamlaka ya ndani ya Wapalestina.

Wao pamoja na nchi nyingine nyingi za Ulaya, wanapinga mipango ya Israel kuzinyakuwa sehemu za eneo linalokaliwa la ukingo wa magharibi wa mto Jordan kama sehemu ya mpango unaopigiwa chapuo na utawala wa Rais wa Marekani, Donald Trump.

Mamlaka ya ndani ya Palestina ambayo inaitaka sehemu ya ukingo wa magharibi wa mto Jordan kuwa taifa lao la baadaye, inapinga hatua hiyo. Marekani bado haijaidhinisha mipango ya kulinyakua eneo hilo.

USA | Präsident Mahmoud Abbas | Sicherheitsrates der Vereinten Nationen in New York
Kiongozi wa Mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas Picha: Getty Images/AFP/J. Eisele

"Tunakubaliana kwamba hatua yoyote ya unyakuaji wa maeneo ya Palestina yaliyochukuliwa mnamo mwaka 1967 itakuwa ni ukiukwaji wa sheria za kimataifa na sio lazima kuweka msingi wa mchakato wa amani,” walisema Mawaziri wa kigeni wa Ulaya na Mashariki ya Kati, baada ya mkutano wao kwa njia ya video na kuongeza kuwa hawatayatambua mabadiliko yoyote ya mipaka ya mwaka 1967 ambayo haikukubaliwa na pande zote mbili kwenye mzozo huo. Hii pia itakuwa na athari kwa mahusiano na Israel.

Israeli ilikataa kutoa kauli kuhusu suala hilo, lakini katika taarifa tofauti, Ofisi ya Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu ilisema kiongozi huyo alimweleza Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson siku ya Jumatatu kuwa amejitolea kwa dhati katika mpango wa ukweli wa Rais Trump kwa eneo hilo.

Taarifa ya Netanyahu ilisema Israel iko tayari kufanya mashauriano kwa msingi wa mpango wa amani wa rais Trump, ambao ni mzuri na unaotekelezeka, na wala haitarejea tena kwenye mifumo ya zamani iliyofeli.