1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mbunge Bobi Wine akamatwa Uganda baada ya dereva wake kuuawa

14 Agosti 2018

Ikiwa yamebaki masaa kadhaa kufanyika uchaguzi wa mdogo katika eneo la Arua nchini Uganda, mbunge Robert Kyagulani Ssentamu maarufu Bobby Wine amekamatwa baada ya dereva wake kuuwawa alipopigwa risasi na polisi. DW imezungumza na mwandishi wa habari na mchambuzi wa masuala ya siasa aliyeko Kampala, Uganda, Kassim Kayira, na hapa anazungumzia kisa hicho.

https://p.dw.com/p/338QW

Mwanamuziki wa Uganda na mbunge wa upinzani Robert Kyagulanyi, anayejulikana zaidi kama Bobi Wine, alikamatwa Jumanne baada ya maafisa wa usalama kumfyatulia risasi na kumuua dereva wake.

"Tumemkamata Bobi Wine na watu wengine asubuhi ya leo na tunae hatiani," amesema  Emilian Kayima, msemaji mkuu wa kikosi cha polisi Uganda.

Kyagulanyi alikamatwa kaskazini-magharibi mwa mji wa Arua ambako alikuwa akiunga mkono kampeni za mgombea mmoja wa upinzania katika uchaguzi huo wenye ushindani mkali ambao haata Rais Yoweri Museveni alionekana kumuunga mkono mmoja wa wagombea wa chama chake tawala. 

Kufuatia mikutano ya kampeni ya pande zote mbili iliyofanywa kwa wakati mmoja Jumatatu, Kayima amesema Kyagulayi alikamatwa kwa kuzuia msafara wa magari wa rais Museveni.

Ili kuhakikisha kunakuwepo usalama, polisi walifyatua risasi za moto kutawanya watu, na kumuua dereva wa  Kyagulanyi.

Katika ukurasa wake wa Twitter na kabla y akutiwa mbaroni na polisi, Kyagulanyi amedai polisi walimuua dereva wake kimakosa.

"Polisi wamempiga risasi na kumuua dereva wangu wakifikiri ni mimi," amesema Kyagulanyi, katika picha aliyoiweka katika mtandao huo ikimuonesha mtu aliyeroa damu katika kiti cha dereva wa gari.

Mgombea wa upinzani Kassiano Wadri pia amekamatwa na polisi.

Uchaguzi huo mdogo wa marudio, unaotarajiwa kufanyika Jumatano, umeitishwa kufuatia kuuawa kwa mbunge wa Manispaa hiyo ya Arua kwa tiketi ya chama tawala, Ibrahim Abiriga baada ya kupigwa risasi mwezi Juni, karibu na nyumba yake huko Mattuga Wilaya ya Wakiso.