1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matokeo ya uchaguzi wa rais Kongo kuanza kutangazwa

21 Desemba 2023

Tume Huru ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo - CENI imesema itaanza kutangaza ijumaa hatua kwa hatua matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatano

https://p.dw.com/p/4aRpu
Wahlen in der DR Kongo
Picha: ARLETTE BASHIZI/REUTERS

Uchaguzi huo ulikamilika jana jioni katika siku ya pili ya upigaji kura kufuatia matatizo ya usafiri na vifaa. Mmoja wa maafisa wakuu wa CENI Didi Manara amesema matokeo ya awali yataanza kuchapishwa leo Ijumaa. Mahakama ya Kikatiba kisha inatarajiwa kutangaza matokeo rasmi mnamo Januari 10.

Soma pia: Kwa nini uchaguzi ni muhimu DR Kongo?

Rais Felix Tshisekedi mwenye umri wa miaka 60 anatafuta muhula wa pili madarakani. Wagombea wakuu, daktari wa wanawake Denis Mukwege, mwenye umri wa miaka 68 na mshindi wa tuzo ya Amani ya Nobel, mfanyabiashara na gavana wa zamani Moise Katumbi mwenye umri wa miaka 58 na Martin Fayulu mwenye umri wa miaka 67, wote wamelalamikia kuwepo hitilafu.

Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo | Uchaguzi 2023
Raia wa Kongo wakionekana katika moja ya vituo vya kupigia kura Kinshasa Picha: JOHN WESSELS/AFP

Wakati zoezi la kuhesabu kura likiwa linaendelea  katika baadhi ya vituo vyakupigia kura nchini DRC, mjini Goma baadhi ya raia waliojitokeza tena kupiga kura wameshindwa kutekeleza haki yao na kurejea majumbani mwao.

Kwenye baadhi ya vituo hapa mjini Goma, tayari zoezi hilo limekamilika huku hesabu za kura zikiwa zinaendelea hadi jioni hii. Mawakala wa wagombea na waangalizi kutoka miungano mbalimbali wanafanya ukaguzi wa majina yalio pigiwa kura. 

Hata hivyo, wananchi waliokosa kushiriki zoezi hilo walijitokeza tena asubuhi ya leo Alhamisi (21.12.2023) kuitikia wito wa CENI iliyotangaza kuongeza muda wa siku moja kwa mchakato huo, lakini hawakuchagua sababu milango ilikuwa tayari imefungwa.
 Chama cha FCC chadai Tshisekedi ameuvuruga uchaguzi wa Kongo

Kwenye kituo cha Faraja katikati mwa mji wa Goma baadhi ya wapiga kura pia waliolala nje ya vituo vya kupigia kura wanadai dosari walizozishuhudia zinawapa wasiwasi kuhusu matokeo ya uchaguzi. 

Waangalizi wakosa kufika katika baadhi ya vituo vya kupigia kura

Wanawake wa Goma wanataka nini kwenya uchaguzi huu?

Zoezi hili  la upigaji kura likiwa limeongezewa muda, mjini Goma hali hiyo imekuwa ni tofauti ambapo wananchi waliomba kuongezewa hata siku mbili za ziada.Katika baadhi ya vituo vya kupigia kura mjini Goma, hakukuwa na waangalizi wakati zoezi hili likiendelea hali iliyowatia mashaka wagombea wa ngazi mbalimbali.

Uchaguzi nchini Kongo waingia siku ya pili

Kura zinaendelea kuhesabiwa katika uchaguzi  huu wa urais unao elezwa kuwa wenye utata  na ambao umegubikwa na changamoto mbalimbali ikiwemo vifaa vibovu vyakupigia kura.

Watu milioni 44 wamejiandikisha kupiga kura katika nchi hiyo yenye jumla ya watu milioni 100.  Matokeo ya uchaguzi yatatangazwa baada ya siku kadhaa.

afp, ap, dpa, reuters