1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama cha National Rally chaangukia pua, matokeo ya Ufaransa

8 Julai 2024

Muungano wa mrengo wa kushoto wa New Popular Front wategemea kutowa waziri mkuu baada ya kutwaa ushindi katika uchaguzi wa bunge nchini Ufaransa

https://p.dw.com/p/4i0mr
Parlamentswahl in Frankreich 2024 | Paris | Kundgebung linker Parteien auf der Place de la République
Picha: Lionel Urman/ABACAPRESS/IMAGO

Nchini Ufaransa, chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha National Rally kimepata pigo kubwa kwa kushindwa katika duru ya pili ya uchaguzi wa bunge, huku muungano wa vyama vya mrengo ya kushoto na muungano wa rais Emmanuel Macron wa siasa za wastani wakiibuka washindi.

Macho yote na masikio hivi sasa yanaelekezwa kwa rais Macron kuona je ni nani atakayemteuwa waziri mkuu?

Muungano mpya wa vyama vya mrengo wa kushoto uliaonzishwa mwezi Juni baada ya rais Emmanuel Macron kutangaza uchaguzi wa bunge wa mapema,wa New Popular Front (NPF) na washirika wake wamejizolea viti 187 katika bunge la Ufaransa la  viti 577 huku muungano wa  siasa za wastani wa rais Macron ukijinyakulia viti 159 na chama cha siasa kali cha National Rally kikiambulia viti 142.

Vyama vyote vyashindwa kupata wingi wa kudhibiti bunge

Hata hivyo vyama vyote hivyo vimeshindwa kupata wingi wa kutosha wa viti 289 vinavyohitajika kupata ushindi wa kuwa na udhibiti wa moja kwa moja wa bunge.

Pamoja na kwamba wananchi wengi wa Ufaransa wameamka wakishusha pumzi ya kuiona ahueni baada ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia kushindwa, wanatambua kwamba kuwepo bunge ambalo halina udhibiti wa moja wa moja wa chama kimoja, pia ni hali inayoweza kuleta  matatizo barani Ulaya.Soma pia: Le Pen asema atapinga wanajeshi wa Ufaransa kupelekwa Ukraine

Rais wa Ufaransa  Emmanuel Macron
Rais Emmanuel MacronPicha: Ludovic Marin/AFP/Getty Images

Muungano wa mrengo wa kushoto wa New Popular Front unaamini sasa ni jukumu lake kutowa waziri mkuu, Marine Tondelier ni kiongozi wa chama cha Kijani ambacho ni sehemu ya muungano wa mrengo wa kushoto.

"Ni jukumu letu kwa kuzingatia muongozo wa kitaasisi, kupata suluhisho. Kwa mujibu wa muongozo wa kitaasisi Emmanuel Macron anapaswa  leo kuwaomba New Popular Front kutoa jina la waziri mkuu.suali ni je atafanya hivyo? Au hatofanya? Kwasababu  rais huyu  siku zote ana mambo mapya. Tutaona lakini huo ndio mtazamo wa kitaasisi.''

Ulaya yashusha pumzi baada ya matokeo

Kushindwa kwa chama cha siasa kali cha Marine Le Pen nchini Ufaransa kumewapa pia faraja viongozi katika nchi nyingine za Umoja wa Ulaya na hasa washirika wa Ukraine waliokuwa wakikhofia kuingia kwa serikali itakayoongozwa na chama hicho,kungemaanisha habari njema kwa Urusi na janga kwa Ukraine.Soma Pia: Wafaransa wapiga kura duru ya pili ya uchaguzi wa Bunge

 Charles Michel, Volodymyr Zelensky na Ursula von der Leyen
Viongozi wa Umoja wa Ulaya na rais wa Ukraine Zelensky katikatiPicha: Olivier Hoslet/AP/picture alliance

Msemaji wa kremlin Dmitry Peskov Urusi hivi sasa inafuatiliwa kwa karibu mchakato wa kuundwa serikali akisema Ufaransa ni nchi muhimu katika Umoja wa Ulaya na kwahivyo kila kitu kinachofanyika katika taifa hilo ni muhimu kwa Urusi.

Makamu wa kansela nchini Ujerumani Robert Habeck amewapongeza Wafaransa  kwa juhudi zao za kuwazuia wenye siasa kali kuingia serikalini.

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW