1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maswali yaibuka kuhusu miili 11 ilopatikana Mto Tana Kenya

13 Septemba 2021

Serikali ya Kenya yakabiliwa na shinikizo kutoka mashirika ya kijamii, viongozi wa dini na kisiasa kutoka Pwani ya Kenya kutoa taarifa kuhusu zaidi ya maiti 11 zilizopatikana zikiwa zimeanza kuoza ndani ya Mto Tana.

https://p.dw.com/p/40Fsr
Orma Patroulie am Tana, Kenia
Picha: Adrian Gregorich

Kwa muda wa miezi mitatu sasa maiti kumi na moja zimeopolewa kutoka mto huo huku baadhi yake zikiwa zimefungiwa kwenye mawe makubwa. Idara ya polisi inasema inafanya uchunguzi wa vinasaba kuweza kuwatambua watu hao ila jambo hilo linakuwa gumu kutokana na miili hiyo kuoza. 

Seneta wa jimbo la Mombasa Mohammed Faki amezikosoa idara za usalama kwa kuwa kimya juu ya jambo hilo ambalo limekuwa kama desturi kwa watu kupotea na baadaye kupatikana wameuliwa kinyama. Kiongozi huyo amesema atapeleka mswada bungeni wa kutaka wizara ya usalama kushurutishwa kuwajibika.

Mjini Mombasa na Lamu familia zimekuwa zikitoa taarifa za watu wao kutekwa nyara, familia hizo kwa sasa zimeombwa kufika katika idara ya usalama na hospitali ya Garisa ili wafanyiwe ukaguzi wa kimaabara ndio ulinganishwe na vinasaba vya maiti hao.

Naibu kiongozi wa baraza kuu la waisilamu nchini Kenya Sheikh Moudhar Khitamy ameitaka serikali kuwajibika katika kadhia hii inayoendelea huku akidai wanaolengwa ni jamii ya Waisilamu. 

Mkuu wa idara ya upelelezi nchini Kenya George Kinoti ametoa taarifa akisema kuwa wameanzisha uchunguzi. 

Mwandishi: Faiz Musa/DW/Mombasa

Mhariri: Iddi Ssessanga