1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Marekani imetangaza msaada wa mwisho wa silaha kwa Ukraine

Hawa Bihoga
28 Desemba 2023

Marekani imetangaza kile ilichokiita msaada wa mwisho uliosalia wa silaha kwa Ukraine chini ya idhini iliopo, huku Bunge la nchi hiyo likihitajika kufanya maamuzi ikiwa litaendelea kuunga mkono vita nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/4aeda
Rais wa Marekani Joe Biden na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika mkutano na waandishi wa habari
Rais wa Marekani Joe Biden na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika mkutano na waandishi wa habariPicha: CHIP SOMODEVILLA/AFP/Getty Images

Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani imesema msaada huo wa mwisho wenye thamani ya dola milioni 250, unajumlisha mifumo ya ulinzi wa anga na makombora.

Rais Joe Biden amefanya kuiunga mkono Ukraine kuwa kipaumbele na silaha za Marekani na msaada wa kifedha umekuwa muhimu katika kuisaidia Ukraine inayoungwa mkono na mataifa ya Magharibi katika vita vyake dhidi ya Urusi.

Hata hivyo Warepublikan wenye msimamo mkali wameongoza juhudi za kuzuwia msaada zaidi wakiwataka Wademokrat wakubali kwanza kupitisha hatua kali za kuzuwia uhamiaji haramu kwenye mpaka wa kusini wa Marekani.