1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUturuki

Uchaguzi Uturuki: Chunguzi za maoni haziaminiki

Erkan Arikan
15 Mei 2023

Siyo usimamizi wake wa tetemeko baya la ardhi wala hali mbaya ya kiuchumi vinaonekana kumdhuru Erdogan katika uchuguzi. Rais huyo anaweza kuaminiwa na wapigakura kubadilisha mambo tena, anasema Erkan Arikan.

https://p.dw.com/p/4RNUQ
Türkei Ankara Erdogan nach Präsidentschaftswahl
Picha: ADEM ALTAN/AFP

Baada ya utawala wa zaidi ya miaka 20 wa Recep Tayyip Erdogan na serikali yake ya chama cha AKP, mabadiliko ya utawala kuelekewa upinzani yalionekana kama jambo la dhahiri zaidi kuliko wakati wowote ule. Lakini kwanza kabisaa kila kitu kinatokea tofauti na pili kuliko unavyoweza kudhani. Rais ajaye wa Jamhuri ya Uturuki ataamuliwa katika duru ya pili.

Erdogan anazidi kuitawala Uturuki kwa mkono wa chuma, na umaarufu wake unapungua, kutokana na hali mbaya ya kiuchumi, ambayo inasababisha kutoridhika kunakoeleweka miongoni mwa raia. Lakini upinzani haukuweza kupata wingi katika duru ya kwanza ya uchaguzi ili kumuweka rais madarakani. Katika muda wa siku 14 zijazo kutakuwa na mpambano kati ya Erdogan na mpinzani wake mkuu Kemal Kilicdaroglu.

"Alieshindwa ni Kilicdaroglu"

Kama mtu angefuata taasisi za uchunguzi wa maoni, mgombea wa upinzani Kemal Kilicdaroglu angepaswa kumshinda Erdogan siku ya Jumapili. "Usiamini taasisi yoyote ya uchunguzi wa maoni," anasema dereva wetu Sedat, anaetwendesha kutoka makao makuu ya AKP kwenda hotelini baada ya saa nne za usiku.

Türkei Bursa | Präsidentschaftswahl | Kemal Kilicdaroglu vor Erdogan Wahlplakat
Mpinzani mkuu wa Erdogan aktika duru ya pili Kemal Kilicdaroglu.Picha: MURAD SEZER/REUTERS

Hakuna anaeleza ukweli katika kampuni hizi. Erdogan yumkini atashinda tena katika duru ya pili. Kilicdaroglu ndiye ameshindwa katika uchaguzi," ansema kwa masikitiko makubwa usoni mwake. "Watu wetu wanaogopa kusema kwa uwazi nani wanamchagua, kwa sababu vinginevyo polisi itakuwa mlangoni siku inayofuata.

Soma pia: Duru ya pili ya uchaguzi wa urais Uturuki kufanyika Mei 28

Bila shaka kila mmoja sasa anajiuliza namna matokeo yalivyokuja. Mgao mdogo wa kura kwa chama cha kizalendo cha IYI haungeweza kumsaidia mgombea wa upinzani Kilicdaroglu. Na zaidi ya hayo, chama kinachounga mkono Wakurdi cha HDP kilisalia chini ya asilimia 10 ya kura.

Hii inaweza kuwa ilitokana na ukweli kwamba, tofauti na uchaguzi uliopita, chama hicho hakikuweka mgombea wake wa urais. Hii ikawafanya wafuasi wake kutokwenda kwenye vituo vya kupigia kura. Wakurdi wengi hawakupendezwa pia na uungwaji mkono wa wazi wa HDP kwa Kilicdaroglu.

Wazalendo na wazalendo wakereketwa waongoza

Kampeni ya uchaguzi, iliyoendeshwa pia kwa msingi wa mzozo wa wakimbizi nchini Uturuki, ilivutia kura katika kambi ya wazalendo. Kikundi hiki kilionekana kwenye asilimia ya chini au hata kwenye safu ya maelfu. Lakini Sinan Ogan, mgombea urais wa mrengo wa kizalendo alipata zaidi ya asilimia 5. Chama cha siasa kali za kizalendo cha MHP, ambacho kilishuka katika kura za maoni hadi asilimia 7, kimeibuka na asilimia 10.

Ahadi ya wazi ya kuwarudisha wakimbizi wengi iwezekanavyo makwao iliwavutia wapigakura nchini Uturuki. Lakini siyo hilo tu. Wakati wa kampeni ya uchaguzi jambo moja lililoshuhudiwa mara kwa mara ni lugha ya vurugu, vitisho na mashambulizi, hasa kutoka kambi ya rais Erdogan.

Türkei Wahlen
Wafuasi wa rais Erdogan wakiwa katika furaha wakati matokeo yakizidi kutolewa.Picha: Kivanc El/DW

Na kama kuna jambo analolimudu vyema Erdogan, ni kuwakashfu wapinzani wake wa kisiasa. Kilicdaroglu atachukuwa maagizo kutoka PKK. Yeye kwa upande mwingine ni tofauti: "Tunachukuwa maagizo kutoka kwa Bwana wetu na watu wetu!", Erdogana alisema kupitia kipaza sauti kwenye roshani ya makao makuu ya chama chake muda mfupi baada ya kupiga kura yake. Na kwenye mikutano ya kampeni, rais huyo alisikika akisema, "Mwamini mcha Mungu kuliko mlevi."

Tetemeko la ardhi na hali ya uchumi hazikuwa sababu

Muda mfupi baada ya tetemeko kubwa la ardhi mwezi Februari mwaka huu, ambapo zaidi ya watu 51,000 walipoteza maisha nchini Uturuki pekee, kila mtu alifikiri kwamba usimamizi mbaya wa mgogoro wa Erdogan ungempa somo katika ngome za AKP ambazo ziko kwenye kitovu cha tetemeko hilo. Lakini hapa pia mambo yalikuwa tofauti.

soma pia: Erdogan aahidi kukabidhi madaraka iwapo atashindwa uchaguzi

AKP na Erdogan hawakurekodi hasara yoyote kubwa katika maeneo hayo. Kura zao zilipungua kwa chini ya asilimia mbili tu. Lakini hiyo pia haikumnufaisha mgombea wa upinzani Kilicdaroglu - mzalendo Sinan Ogan ndiye alifaidika hapa.

Hata hali mbaya ya kiuchumi na mfumuko wa bei wa juu, ukosefu zaidi wa ajira na tatizo kubwa la wahitimu wa vyuo vikuu kukimbilia nje havikumdhuru Erdogan. Inavyoonekana, wengi wanaamini kuwa rais huyo aliyeko madarakani anaweza kubadilisha mambo na kuirejesha Uturuki kwenye mkondo sahihi kiuchumi.

Mzalendo Ogan ashikilia karata ya ushindi

Katika siku 14 zijazo, macho sasa yataelekezwa kwa mzalendo Sinan Ogan. Mtazamo wa mbunge huyo wa zamani wa chama cha mrengo wa kulia cha MHP unawiana kwa karibu na muungano wa Erdogan wa vyama vya kihafidhina.

Ogan sasa ana kadi zote mkononi mwake. Akiwa na zaidi ya asilimia 5, anaweza kuketi na kusubiri kuona ni mapendekezo yepi serikali na upinzani wanaweza kutoa. Kwa sababu miungano yote miwili inajua kuwa hakuna njia ya kumkwepa Ogan.

Licha ya Ogan kumkosoa vikali Erdogan huko nyuma, haimaanishi kwamba Kilicdaroglu anaweza kuwa na uhakika wa kuungwa mkono na Ogan. Kama nilivyosema: Kwanza mambo huwa tofauti, na pili, kuliko unavyofikiria.

Mkala hii imetafisiriwa kutoka Kijerumani