1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoCameroon

Manchester United yamsaini Onana kwa mkataba wa miaka mitano

21 Julai 2023

Mlinda lango Andre Onana amejiunga na Manchester United kwa mkataba wa miaka mitano hadi Juni mwaka 2028, kukiwa na kipengee cha kuongeza mwaka mmoja zaidi.

https://p.dw.com/p/4UDgG
WM in Katar 2022 I Kamerun v Serbien
Mlinda lango wa timu ya taifa ya Cameroon Andre OnanaPicha: Sipa USA/IMAGO

Mashetani Wekundu wamekamilisha usajili wa Andre Onana baada ya kutoa pauni milioni 51 kwa Inter Milan.

"Kujiunga na Manchester United ni heshima kubwa na nimefanya kazi kwa bidii maishani mwangu kufikia hatua hii, kukwepa vizuizi vingi njiani,” ameeleza Onana.

Mlinda lango huyo sasa atajiunga na wachezaji wenzake katika ziara ya maandalizi ya kuelekea msimu mpya.

Manchester United inajifua kwa mechi za kirafiki nchini Marekani.

Raia huyo wa Cameroon amecheza mechi 255 katika ngazi ya klabu na kutoruhusu kufungwa bao katika mechi 104.

Onana amewahi kushinda mataji matatu ya Ligi Kuu ya Uholanzi na makombe mawili ya KNVB akiwa na Ajax kabla ya kujiunga na Inter Milan mwaka 2022.

Msimu uliopita, alishinda kombe la Coppa Italia na kuwa mlinda lango aliyeruhusu magoli machache katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Champions League.