1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makamu wa Rais wa Marekani ziarani barani Afrika

Angela Mdungu
25 Machi 2023

Makamu wa Rais wa Marekani Kamala Harris, anaanza ziara yake ya wiki moja barani Afrika katika juhudi za kuboresha mahusiano kati ya nchi yake na bara hilo.

https://p.dw.com/p/4PEzj
USA Kamala Harris Afrika-Gipfel
Picha: Andrew Harnik/AP Photo/picture alliance

Ziara ya Harris barani Afrika ndiyo ya karibuni zaidi kufanywa na kiongozi wa ngazi ya juu wa Marekani wakati utawala wa wa Rais Joe Biden ukijaribu kukabiliana na ushawishi wa China unaokua barani humo.

Katika ziara hiyo, Kamala Harris anatarajiwa kuzitembelea nchi za Ghana, Tanzania na Zambia, huku akiangazia zaidi maendeleo ya kiuchumi, mabadiliko ya tabia nchi, usalama wa chakula na ongezeko la idadi ya vijana.

Anatarajiwa kuwasili katika mji mkuu wa Ghana, Accra, Jumapili.

Anapanga kukutana na viongozi wa kila nchi atakayotembelea na kuweka shada la maua katika ubalozi wa Marekani jijini Dar es Slaam, ambako lilifanyika shambulizi la bomu mwaka 1998.