1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMalawi

Makamu wa Rais wa Malawi afariki dunia katika ajali ya ndege

11 Juni 2024

Dr. Saulos Chilima, ni miongoni mwa watu 10 waliokufa katika ajali ya ndege ndogo ya kijeshi iyoanguka katika eneo la milima kaskazini mwa nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/4gv7F
Rais wa Malawi atangaza rasmi kifo cha makamu wake  Saulos Chilima katika ajali ya ndege
Rais wa Malawi atangaza rasmi kifo cha makamu wake Saulos Chilima katika ajali ya ndegePicha: Reuters TV/REUTERS

Rais Lazaro Chakwera alitangaza katika hotuba ya moja kwa moja kwenye televisheni ya taifa kwamba mabaki ya ndege hiyo yalipatikana baada ya kuitafuta kwa zaidi ya siku moja katika msitu mnene ulioko eneo milima karibu na mji wa kaskazini wa Mzuzu.

Chakwera alisema hakuna mtu aliyenusurika ajali hiyo.

"Maneno hayawezi kueleza jinsi tukio hili linavyotuhuzunisha nafikiria juu ya uchungu tulionao na tukaokuwanao sote katika siku na wiki zijazo tunapoomboleza msiba huu mbaya. Ni muhimu tuendelee kufarijiana wakati tunapoomboleza kwa pamoja. Dr Saulos Chilima alikuwa mtu mwema, baba mzuri na mume aliyejitolea, raia mzalendo aliyeitumikia nchi yake kwa upendo, na makamu wa rais asiye na mfano. Ni heshima kubwa maishani mwangu kufanyakazi na yeye kama naibu wangu na mshauri wangu pia kwa miaka minne iliyopita.” alisema Chikwera.

Bibi Shanil Dzimbiri, mke wa Rais wa zamaniwa Malawi Bakili Muluzi, pia alikuwa ndani ya ndege hiyo. Chakwera amesema kulikuwa na abiria saba na wafanyakazi watatu wanajeshi kwenye ndege hiyo.

Kundi hilo lilikuwa likisafiri kuelekea Mzuzu kuhudhuria mazishi ya waziri wa zamani. Dr. Chilima amefariki akiwa na umri wa miaka 51 alikuwa amerejea kutoka katika kwenye ziara rasmi nchini Korea Kusini siku ya Jumapili.