Makaburi yenye maiti 5,400 yagunduliwa Rwanda
21 Septemba 2018Matangazo
Maafisa nchini Rwanda wamegundua maiti za wahanga 5, 400 wa mauaji ya kimbari ya 1994.
Kwa mujibu wa Naphtal Ahishakiye, Katibu mtendaji wa IBUKA, Jumuiya ya walionusurika na mauaji ya kimbari, maiti hizo zilifukuliwa kutoka makaburi 26 ya halaiki katika wilaya za Masaka na Kicukiro (KICHUKIRO) za mji mkuu Kigali.
Mkaazi mmoja wa Kicukiro ambaye alishuhudia mauaji hayo aliwaeleza maafisa juu ya makaburi hayo ya halaiki ambayo hayakuwa yakijulikana hapo kabla.
Ahishakiye alisema msako wa makaburi zaidi katika wilaya hiyo hiyo, unaendelea. Maiti zipatazo 18,000 zimegunduliwa tokea mwezi Aprili.
Mnamo mwaka 1994, zaidi ya Watutsi na Wahutu 800,000 waliokuwa na msimamo wa wastani waliuwawa katika kipindi cha siku 100.