Maisha ya wahamiaji Israel ni ya mashaka
25 Mei 2012Serikali ya taifa hilo ikiwatazama wahamiaji kutoka Afrika ni hatari kwa Wayahudi.
Wahamiaji hao wanaoingia katika makundi ya watu elfu kwa mwezi wamekuwa wanaingia nchini humo katika kipindi cha miaka saba iliyopita tu na kwa sasa Israeli ina wahamiaji wanaokaribia elfu sitini kutoka Sudan na Eritrea pekee.'
Wahamiaji hao wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya uzalilishaji kama vile ubakaji, kupigwa na kuuwawa. Serikali ya Israel ikiwanyima muda wa kutosha kuweza kuishi kwa kuwapa vibali vya muda mfupi.
Vijana wenye asili ya Afrika hujikusanya katika eneo la levisky Park na kuwangoja watu wa kuwapa vibarua. Huyu hapa ni miongoni mwao
" Watu wengi wanakuja hapa na wengine wanapata kazi za siku au za juma moja. Wengine wanapewa vibali lakini vibali hivyo haviturusu kufanya kazi, kupata matibabu na huduma nyingine." anasema kijana katika jiji la Tel-Aviv
Huku wahamiaji haramu nao wakiingia nchini humo kupitia Rasi ya Sinai hasa baada ya kuangushwa kwa utawala waaliyekuwa Rais wa Misri Hosni Mubarak mwaka jana. Hali hii imefanya Israei kujenga ukuta wa Kilometa 200 kuwazuia kuingia. Wahamiaji wote kutoka Afrika wanatazamwa kama wahalifu.
Kijana Mohammed, yeye yu njia panda akitokea Eritrea miezi minne iliyopita
"Kama hauna kazi hauwezi kupata usingizi, kila mara ni wasiwasi tu. Hauwezi kubadilisha mavazi. Nia yangu ni kusoma, baadae ndiyo nifanye kazi. Wananicheka kuwa sina mkono lakini mimi ni sawa na watu wengine." alisema kwa uchungu kijana Mohammed.
Kauli ya Waziri Mkuu wa Israel
Hali ya mashaka ya wahamiaji hao inawekwa msumari wa moto na kauli ya Waziri Mkuu wa Israel ambaye ameonya kuwa wahamiaji hao 60,000 watafikia laki sita na kutishia kizazi cha wayahudi muda si mrefu.
Hali hii imefanya Marekani kuipinga Israel kwa ubaguzi huo ambapo kwa mwaka 2011watu 3692 waliomba vibali vya hifadhi ya ukimbizi lakini alikubaliwa muhamiaji mmoja tu.
Mwandishi:Adeladius Makwega/APE
Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman