1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya ECJ: FIFA na UEFA zilitumia vibaya nafasi zao

27 Mei 2024

FIFA, na UEFA "walitumia vibaya nafasi zao kuu" na "kuzuia ushindani" kwa kukataa kuundwa kwa Ligi mpya ya Ulaya "Super League" uamuzi uliotolewa na mahakama moja nchini Uhispania leo Jumatatu:

https://p.dw.com/p/4gLZf
Nyundo inayotumiwa na majaji juu ya bendera ya Umoja wa Ulaya
Nyundo inayotumiwa na majaji juu ya bendera ya Umoja wa UlayaPicha: DesignIt/Zoonar/picture alliance

Shirikisho la Soka Duniani, FIFA, na Shirikisho la Kandanda barani Ulaya, UEFA "walitumia vibaya nafasi zao kuu" na "kuzuia ushindani" kwa kukataa kuundwa kwa Ligi mpya ya Ulaya "Super League". Hayo yameelezwa katika uamuzi uliotolewa na mahakama moja ya nchini Uhispania leo Jumatatu.

Mahakama hiyo imesema kwamba FIFA na UEFA wameweka "vizuizi visivyo na sababu na visivyo na uwiano" kwa ushindani huru ndani ya soko la kandanda.

Miamba wa kandanda Real Madrid na Barcelona wanaunga mkono pakubwa mradi huo ambao unapingwa na vilabu vingi vikubwa vya Ulaya.

Soma pia: Paredi la ubingwa lasimamisha shughuli mjini Leverkusen 

Uamuzi wa leo umeunga mkono ule wa awali wa Mahakama ya Haki ya Ulaya (ECJ) ambayo iliamuru wadau hao wakuu "kukomesha kile ilichokiita tabia ya kupinga ushindani". Kesi hiyo ilifikishwa mahamakamani na wadhamini na wapiga debe wa Ligi kuu ya Europa, A22 Sports Management.

A22 walichipuka baada ya uamuzi wa Mahakama ya Haki ya Umoja wa Ulaya (ECJ) mnamo Desemba 2023, ambayo pia iliamua kwamba kufungiwa kwa Ligi Kuu ya Europa ni kinyume na sheria za Ulaya, uamuzi ambao pia uligundua kuwa UEFA haikuwa na vigezo vilivyo wazi kuidhinisha au kutoidhinisha mashindano mapya.

Hata hivyo, uamuzi huo wa mahakama hautoi picha kamili juu ya uzito wake, kwani unazingatia kanuni ambazo zimeandikwa upya kabisa katika kipindi mpito kusubiri uamuzi. Hatua za muda ziliwekwa kuzuia FIFA na UEFA kuingilia au kuchukua hatua kuhusiana na mradi huu.

Wachezaji wa klabu ya Barcelona ya wanawake wakisheherekea ushindi
Wachezaji wa klabu ya Barcelona ya wanawake wakisheherekea ushindiPicha: Goal Sports Images/IMAGO

"Haiwezekani kuweka katazo au kizuizi kama suala la kanuni, kwa maneno mengine kukataza mradi mwingine wowote katika siku zijazo," alielezea Hakimu Sofia Gil Garcia katika uamuzi wake wa Jumatatu, ulionukuliwa na shirika la habari la AFP.

"Kukubali kinyume chake itakuwa sawa na kukubali aina ya marufuku ... kwenye mradi wowote wa mashindano ya kandanda ambao unashindana na Ligi ya Mabingwa ya sasa," aliendelea hakimu huyo.

Uhispania haikuwa miongoni mwa mataifa 26 ya Ulaya ambayo yalitia saini tamko la pamoja dhidi ya miradi kama vile Ligi kuu ya Europa mwezi Februari, ikisisitiza haja ya ushindani ulio "wazi".

Soma pia: FIFA kujadili pendekezo la kuisimamisha Israel soka la kimataifa

Rasimu ya kwanza ya mradi wa Ligi kuu ya Europa uliopendekezwa mwaka wa 2021 na wataalam wa kandanda katika vilabu kumi na mbili vya Ulaya, ikiwa ni pamoja na Real Madrid na Barcelona, haukuungwa mkono, hasa kutokana na upinzani mkali kutoka kwa mashabiki wa klabu za Uingereza na vitisho kutoka kwa UEFA na FIFA.

Hata hivyo, mradi huo ulizinduliwa upya mapema mwaka huu baada ya ECJ kuamua kwamba mamlaka ya wadau hawa wawili wakuu "hayana vigezo vyovyote vinavyohakikisha kuwa yanazingatia uwazi, yana malengo mazuri, yana uwiano na hayabagui".

Wakati huo huo,UEFA imesahihisha 'upungufu' huu kwa kanuni mpya, zenye maelezo zaidi zilizopitishwa mnamo Juni 2022. Ikijibu uamuzi wa leo wa ECJ, UEFA imesema, "hukumu hii haimaanishi kuwa kile kinachoitwa 'Ligi kuu ya Europa' kimeidhinishwa au kuthibitishwa".

Mkuu wa La Liga Javier Tebas, amepinga vikali mradi wa Ligi hiyo akisema kuwa "uamuzi huo sio wa mwisho, wala hauleti lolote jipya la maana,".