1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaPakistan

Mahakama ya Islamabad yasitisha hatia ya ufisadi kwa Khan

29 Agosti 2023

Mahakama ya juu ya Pakistan imesitisha hatia ya ufisadi dhidi ya Imran Khan pamoja na kifungo cha miaka mitatu gerezani, katika ushindi wa kisheria kwa waziri mkuu huyo wa zamani.

https://p.dw.com/p/4VhQB
Pakistan | Protest gegen die Verhaftung von Imran Khan
Picha: Asif Hassan/AFP/Getty Images

Msemaji wa chama cha Khan cha Pakistan Tehreek-e-Insaf (PTI) amesema mahakama ya juu ya mjini Islamabad, ilibatilisha uamuzi wa mahakama ya chini uliotolewa mwezi huu wa kumfunga jela khan kwa miaka mitatu hatua ambayo ilimuondolea haki ya kugombea katika uchaguzi mkuu ujao. 

Pakistan: Adhabu ya Imran Khan yasimamishwa

Mawakili wake wamesema mteja wao amepewa dhamana  lakini wanahofia kuwa Khan mwenye umri wa miaka 70 huenda akakamatwa tena akihusishwa na moja ya zaidi ya kesi 200 zinazomkabili tangu alipoondoka madarakani mwezi Aprili mwaka 2022. 

"Tumewasilisha ombi tofauti mahakamani kuiomba kutoa amri ya kuipiga marufuku mamlaka ya Pakistan kumkamata Khan kwa kesi yoyote ile." alisema Gohar Khan, moja ya mawili wake alipozungumza na shirika la habari la AFP. 

Uamuzi umekuja baada ya Khan kuhukumiwa miaka mitatu jela

Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistan Imran Khan
Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistan Imran KhanPicha: Akhtar Soomro/REUTERS

Uamuzi huo umekuja wiki kadhaa baada ya khan kushitakiwa na kuhukumiwa miaka mitatu jela na mahakama nyengine, baada ya kumkuta na hatia ya kuficha Mali, baada ya kuuza zawadi za taifa alizokuwa anapokea wakati akiwa madarakani. Imran Khan aliondolewa madarakani kupitia kura ya kutokuwa na imani nae, iliyopigwa bungeni mwaka uliyopita. 

Imran Khan afutiwa mashitaka ya mauaji

Kwa upande wake mtaalamu wa masuala ya kisiasa nchini humo Omar Quraishi aliiambia AFP kwamba kinachosubiriwa sasa ni kuona iwapo Khan ataachiwa kweli na ni lini hasa hatua hiyo itakapochukuliwa kutokana na uzito wa kesi hizo nyengine zinazomkabili. 

Hata hivyo Khan aliyemaarufu sana nchini humo alisema madai dhidi yake na kuondolewa kwake madarakani ni njama ya kumuua kisiasa na imepangwa na jeshi lililo na nguvu Pakistan ili kumyima kugombea muhula  mwengine.  

Serikali yadaiwa kutumia sheria kali kuisambaratisha PTI

Khan alifungwa jela kwa muda mfupi mwezi May kufuatia madai hayo ya ufisadi hatua iliyosababisha vurugu kwa siku kadhaa, na tangu wakati huo chama chake cha PTI kimekuwa kikilengwa na wanachama wake wengi kukamatwa. 

Pakistan Shehbaz Sharif
Waziri Mkuu wa Pakistan Shehbaz SharifPicha: Fabrice Coffrini/AFP

Makundi ya kutetea haki za binaadamu nayo yakapaza sauti zao juu ya hili na kusema kuwa serikali inatumia sheria kali zaidi za ugaidi kukisambaratisha chama hicho huku mashirika ya habari ya ndani ya nchi yakiripoti kupata shinikizo kutoripoti matukio yanayoendeshwa na chama hicho na kumpaka tope kiongozi wake. 

Kiongozi wa upinzani akamatwa Pakistan kwa kosa la kufichua siri za serikali

Kiongozi wa upinzani akamatwa Pakistan kwa kosa la kufichua siri za serikaliWakati Khan alipokamatwa mwezi huu, bunge la taifa hilo lilivunjwa kufuatia ombi la mrithi wake Shehbaz Sharif  ili kutoa nafasi ya serikali ya mpito hadi pale uchaguzi utakapofanyika ndani ya siku 90 baada ya bunge kuvunjwa. Bado tarehe ya uchaguzi huo haijatangazwa. 

Chanzo: ap/afp/reuters