1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMisri

Mahakama Misri yaidhinisha kifungo cha mwanasiasa maarufu

28 Mei 2024

Mahakama ya rufaa nchini Misri imeidhinisha hukumu ya kifungo cha mwaka mmoja jela dhidi ya mwanaharakati maarufu wa kisiasa aliyejaribu kumpinga Rais Abdel Fattah al-Sissi katika uchaguzi wa mwaka wa 2023.

https://p.dw.com/p/4gM5p
Ahmad al-Tantawi
Aliyekuwa mgombea wa urais Ahmad al-Tantawi alipewa kifungo cha mwaka mmoja jelaPicha: Ahmed Hasan/AFP

Mgombea wa zamani wa urais Ahmed Altantawy aliwekwa kizuizini na vikosi vya usalama katika mahakama hiyo mjini Cairo baada ya uamuzi huo. Wakili wake Khaled Ali ameyasema hayo.

Altantawy alipatikana na hatia na kuhukumiwa Februari 2024 pamoja na wasaidizi wake 22, akiwemo msimamizi wa kampeni zake, kwa mashitaka ya kusambaza fomu zisizoruhusiwa za kuidhinisha kugombea kwake.

Mahakama hiyo pia ilimzuia Altantawy kushiriki uchaguzi wa kitaifa kwa miaka mitano ijayo. Mwanasiasa huyo alikuwa ameachiwa kwa dhamana wakati wa kesi hiyo ya rufaa.

Altantawy, ambaye alionekana na wengi kuwa mgombea halisi wa upinzani, alijiondoa katika mbio za urais mwaka jana baada ya kushindwa kupata idadi ya sahihi kutoka kwa wapiga kura inayohitajika ili kupewa uteuzi.

Sissi alishinda karibu asilimia 90 ya kura, kwa mujibu wa Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi nchini Misri. Alishinda muhula wa tatu madarakani ambao utakamilika mwaka wa 2030.