1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magufuli awaonya makandarasi wanaochelewesha miradi

George Njogopa24 Februari 2021

Rais John Magufuli wa Tanzania amezindua barabara ya juu eneo la Ubungo na pamoja na kituo cha kimataifa cha mabasi huku akiwaonya makandarasi dhidi ya kuchelewesha miradi ya serikali kwa kusingizia janga la corona.

https://p.dw.com/p/3pmxs
Tansania Dar es Salaam | Einweihung moderner internationaler Busstand am Mbezi Luis
Picha: Eric Boniphace/DW

Barabara hiyo ambayo ni ya kwanza kushuhudiwa nchini inatazamwa kama ni kiunganishi muhimu kwa wakaazi wa jiji hili na mikoa mingine inayotumia kiunganishi hicho kufanya safari zao ndani ya Dar es Salaam, jiji kubwa kabisa la kiuchumi na kibiashara katika eneo zima la Afrika Mashariki likiwa na wakaazi zaidi ya milioni sita.

Benki ya Dunia ilitowa mkopo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo iliyopewa jina la John Kijazi, aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi ambaye amefariki dunia wiki iliyopita, akiwa miongoni watu kadhaa mashuhuri waliopoteza maisha ndani ya siku za hivi karibuni.

Tansania Dar es Salaam | Einweihung moderner internationaler Busstand am Mbezi Luis
Kiuto kipya cha mabasi kilichojengwa Mbezi Luis, Dar es Salaam.Picha: Eric Boniphace/DW

Akizungumza kwenye uzinduzi wa barabara hiyo iliyoko kwenye maunganiko ya Barabara ya Sam Nujoma na Ubungo, Rais Maguliamesema kukamilika kwake kunaandika historia mpya ya jiji la Dar es Salaam ambalo limepata kuwa makao makuu ya nchi kwa zaidi ya miaka 60.

Amesema daraja hilo siyo tu kwamba limeondoa adha na kero ya muda mrefu ya foleni, lakini pia linatoa picha halisi kuwa Dar es Salaam ni jiji la kibiashara. "Ni laazima dar es Salaam liwe jiji kweli la kisasa, ni laazima ibaki kuwa paliwahi kuwa makao makuu ya serikali yetu."

Soma pia: CCM yasema Rais Magufuli kutoongeza muda madarakani

Kukamilika kwa ujenzi wa daraja hili ni sehemu tu ya hatua nyingine zinazoendelea kuchukuliwa na serikali na uboreshaji wa miundombinu ya barabara na madaraja ya juu na hivi sasa mradi mwingine wa ujenzi wa barabara ya njia nane unaendelea kutekelezwa katika eneo la Pwani.

Kwa kiasi kikubwa miradi hiyo inaendelea kulifanya jiji la Dar es Salaam kuwa la aina yake na kwa mtazamo wa Rais Magufuli miradi kama hii inalifanya jiji hili kukaribiana kabisa na baadhi ya mitaa ya nchi za Magharibi.

John Magufuli of Tanzania
Mradi mwingine mkubwa unaoendelezwa na utawala wa rais Magufuli ni reli ya kisasa.Picha: DW/G.Njogopa

Hata hivyo, Rais Magufuli ametumia fursa hiyo kuwaonya wakandarasi wanaofanya shughuli zao kwa kusuasasua akisema siku zao sasa zinahesabika.

Mbali ya kuzinduliwa kwa barabara hiyo, Magufuli ambaye amepata kuwa waziri wa ujenzi kwa miaka mingi, amezindua kitua kipya cha kisasa cha mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani.

Kituo hicho kilichojengwa eneo la Kimara nje kidogo ya katikati ya jiji, kinajumuisha pia maeneo ya wafanyabiashara ndogondogo na wale wakubwa.