1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoBrazil

Maelfu wamuaga Pele

2 Januari 2023

Hali ya huzuni imetanda nchini Brazil katika hafla ya kumuaga nguli wa soka duniani Pele katika uwanja wa klabu ya Santos, alikoanzia soka lake.

https://p.dw.com/p/4LeJW
Brasilien Pele wurde im Stadion von Sao Paulo aufgebahrt
Picha: Matias Delacroix/AP Photo/picture alliance

Mamia ya mashabiki wanaendelea kuwasili katika uwanja wa Villa Belmiro, uwanja wa nyumbani wa klabu ya Santos, ambapo jeneza la Pele limelazwa, kabla ya kuzikwa kesho Jumanne.

Jaji wa mahakama kuu ya Brazil Gilmar Mendes ambaye ni mmoja wa waombolezaji amemtaja Pele kama shujaa wa taifa. Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva pamoja na viongozi wengine akiwemo Rais wa shirikisho la soka duniani Gianni Infantino wanatarajiwa pia kuhudhuria hafla hiyo ya kumuaga Pele.

Gwiji huyo wa soka wa Brazil alifariki siku ya Alhamisi baada ya kuugua ugonjwa wa saratani ya utumbo. Alikuwa na umri wa 82.

Mazishi yake yanatarajiwa kufanyika kuanzia kesho saa nne asubuhi na atazikwa katika makaburi yaliyoko umbali wa mitaa 600 kutoka uwanja huo.