1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron atoa wito kuimarisha ushirikiano na Asia ya Kati

1 Novemba 2023

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema anataka "kuongeza ushirikiano" na Kazakhstan siku ya Jumatano, kama sehemu ya ziara ya kuimarisha ushawishi wa Ufaransa katika kanda ya Asia ya Kati.

https://p.dw.com/p/4YI2y
Kazakhstan Astana | Ziara ya Rais Macron
Rais wa Kazakhstan Kassym-Jomart Tokayev na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron wakihudhuria mkutano wa habari kufuatia mazungumzo yao mjini Astana, Kazakhstan, Novemba 1, 2023.Picha: President of Kazakhstan/REUTERS

Rais Macron alisema madhumuni ya safari yake ni "kuimarisha ... kukamilisha na kuongeza kasi" ushirikiano wa Ufaransa na Kazakhstan wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika mji mkuu Astana.

Asia ya Kati, ambayo kwa muda mrefu imekuwa chini ya ushawishi wa Urusi na ilikuwa sehemu ya Muungano wa Kisovieti, inapata nadhari zaidi kutoka mataifa mengine huku Moscow ikikabiliwa na vita vyake nchini Ukraine.

Macron alikiri "shinikizo la kijiografia" linalowekwa kwa Kazakhstan, ambayo inapakana na Urusi kaskazini mwake na China mashariki mwake.

"Sipuuzii ugumu wa siasa za kijiografia, mashinikizo, wakati mwingine mivutano ambayo unaweza kukabiliwa nayo," Macron alimwambia rais wa Kazakhstan Kassym-Jomart Tokayev.

"Katika ulimwengu ambapo mataifa makubwa yanataka kuwa watawala na ambapo madola ya kikanda yanakuwa hayatabiriki," rais wa Ufaransa alisema anakaribisha "kukataa kwa Kazakhstan ... kuchukua njia ya kuwa kibaraka."

Soma pia: Kazakhstan yataifisha kampuni baada ya mkasa wa moto mgodini

Tokayev kwa upande wake alisema Ufaransa ilikuwa "mshirika mkuu na wa kutegemewa wa nchi yake katika Umoja wa Ulaya" na kwamba alitaka kutoa ushirikiano wao "msukumo wa ziada".

Kazakhstan Astana | Ziara ya Rais Macron
Rais wa Kazakhstan Kassym-Jomart Tokayev, kushoto, na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, wakikagua gwaride la heshima katika Kaskri la Rais mjini Astana, Novemba 1, 2023.Picha: LUDOVIC MARIN/AFP

Viongozi hao wawili wametia saini makubaliano kadhaa katika sekta kuanzia madini na nishati hadi famasia na usafiri wa anga.

Kampuni kubwa ya nishati ya Ufaransa EDF, iko mbioni kujenga mtambo wa kwanza wa nishati ya nyuklia wa Kazakhstan, mradi ambao utaaamuliwa katika kura ya maoni mwaka huu.

Madini muhimu kwa teknolojia safi, ambayo kanda hiyo inayo kwa wingi, ni sehemu muhimu ya majadiliano.

Ufaransa ndiyo mwekezaji wa tano kwa ukubwa wa kigeni nchini Kazakhstan, ikiwa mbele ya China, kutokana hasa na ushiriki wa kampuni ya nishati ya TotalEnergies katika mradi mkubwa wa visima vya mafuta wa Kashagon.

Biashara kati ya mataifa hayo mawili ilifikia euro bilioni 5.3 mwaka 2022, na Kazakhstan inatoa karibu asilimia 40 ya mahitaji ya urani ya Ufaransa.

Asia ya Kati, ambayo kwa muda mrefu imekuwa chini ya ushawishi wa Urusi na ilikuwa sehemu ya Muungano wa Kisovieti, inavutai nadhari zaidi kutoka mataifa mengine huku Moscow ikijishughulisha na vita vyake nchini Ukraine.

Juhudi za kuimarisha ushawishi ya Asia ya Kati

Kiongozi huyo wa Ufaransa baadaye atasafiri hadi nchi jirani ya Uzbekistan, na kuongeza juhudi za kuimarisha ushawishi wa nchi yake kisiasa na kiuchumi katika eneo hilo lenye utajiri wa nishati.

Soma pia:Rais wa Kazakhstan Kassym-Jomart Tokayev alivunja bunge 

China iko mashughuli hasa katika Asia ya Kati ya mradi wake wa miundombinu ya barabara na reli, lakini Ulaya na Uturuki pia zimeonyesha shauku inayoongezeka katika kanda hiyo.

Waziri Mkuu wa Hungary Viktor Orban na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan wanatarajiwa kuzuru Astana siku ya Alhamisi na Ijumaa, muda mfupi baada ya Macron.

Kazakhstan na Uzbekistan zinalenga uwazi zaidi wa kiuchumi na diplomasia iliyosawazishwa, ingawa Urusi inasalia kuwa mshirika wao mkuu.

TotalEnergies
Kampuni ya niashti ya Ufaransa, ya TotalEnergies ni mmoja ya wawekezaji wakubwa nchini Kazakhstan.Picha: Sebastian Gabsch/Future Image/IMAGO

Kazakhstan ni sehemu ya Shirika la Mkataba wa Usalama wa Pamoja (CSTO) -- muungano wa kijeshi unaoongozwa na Moscow -- pamoja na mataifa mengine mawili ya Asia ya kati, Kyrgyzstan na Tajikistan.

Kremlin ilisema Jumatano kwamba ilidumisha ushirikiano "wa kihistoria" na mshirika wake Astana.

"Kazakhstan ni taifa huru ambalo linaendeleza uhusiano na nchi zingine kwa hiari yake," msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov aliwaambia waandishi wa habari Jumatano alipoulizwa ikiwa Urusi ina wasiwasi na ziara ya Macron.

Suala la utawala wa kisheria na demokrasia

Safari ya Kazakhstan na Uzbekistan inalenga kuunga mkono "maslahi katika mseto wa ushirikiano ulioonyeshwa na nchi zote mbili", duru kutoka ofisi ya Rais wa Ufaransa ilisema.

Marais kadhaa wa Ufaransa wametembelea Kazakhstan tangu kuanguka kwa Umoja wa Kisovieti, lakini Macron atakuwa wa kwanza kwenda Uzbekistan tangu 1994.

Soma pia: Putin adai ushindi katika kulinda Kazakhstan dhidi ya uasi

Licha ya shauku yao ya wazi ya ukombozi wa kisiasa, nchi zote mbili ni mataifa yanayotawaliwa kimabavu ambapo maandamano mara nyingi hukandamizwa kwa nguvu.

Rais wa Uzbekistan Shavkat Mirziyoyev amemaliza miongo miwili ya kutengwa iliyowekwa na mtangulizi wake na mwalimu wake wa zamani Islam Karimov, lakini bado hakuna upinzani wa kweli wa kisiasa.

Macron anapendelea kusisitiza "mvuto wa mageuzi" unaoendelea nchini humo na amesema kuwa suala la utawala wa sheria litaibuliwa wakati wa ziara yake.

Chanzo: Mashirika