1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ligi ya mabingwa barani Ulaya kundi F ni la kifo

Sekione Kitojo
30 Agosti 2019

Barcelona italazimika kupitia shughuli ya kuidhibiti Borussia Dortmund na Inter Milan baada ya mabingwa watatu wa zamani wote kuja pmoja katika kundi F katika upangaji wa makundi uliofanywa siku ya Alhamis mjini Monaco.

https://p.dw.com/p/3OlIn
Monaco | Soccer Champions League Draw
Picha: picture-alliance/dpa/AP Photo/D. Cole

Mabingwa watetezi Liverpool wana miadi na  SSC Napoli tena. Barcelona , Dortmund  na Inter, wakiwa kwa jumla zimeshinda  mara  tisa vikombe vya Ulaya baina yao, wamewekwa pamoja  katika  kundi F pamoja  na mabingwa  wa Jamhuri ya  Cheki Slavia Prague.

Baada ya kupokea  kipigo dhidi ya  Liverpool msimu uliopita, Lionel Messi na  Barcelona wanaendelea  kuwa  timu  inayopigiwa  upatu kusonga mbele wakati  wakiwania  taji lao la  kwanza  la  Champions League tangu mwaka  2015.

CL- Auslosung | Zettel mit dem Aufschrift von Bayern München
Upangaji wa makundi mjini Monaco (29.08.2019)Picha: Getty Images/AFP/V. Hache

Dortmund  ilishinda  taji  hilo mwaka  1997 na  kushindwa  katika fainali  ya  mwaka 2013. Ikiwa  sasa  inapata mafunzo kutoka  kwa kocha  Antonio Conte, Inter Milan iliishinda  Barcelona  katika  nusu fainali  kuelekea ushindi wa hivi  karibuni  kabisa  wa  mataji  yake matatu mwaka  2010.

"Hili  kwa  kweli  ni  kundi  gumu  sana, ambalo linaifanya  kuwa changamoto  kubwa  zaidi kwetu,"  amesema kocha  wa  Dortmund , Lucien Favre.

Liverpool ilisonga mbele katika  kundi  lake  kwa  gharama  ya  Napoli msimu  uliopita  na  kufanikiwa  kulinyakua  taji  hilo , likiwa  taji  lake la  nne  katika  historia  ya  klabu  hiyo mjini  Madrid, na  kikosi  cha Carlo  Ancelotti sasa  kina  fursa  kwa  mara  nyingine  tena  ya kulipa  kisasi.

Vilabu  vyote  hivyo vinatarajiwa  kusonga  mbele  kutoka  kundi E, ambalo linakamilishwa  na  mabingwa  wa  Austria Salzburg  na Genk  ya  Ubelgiji.

UEFA Champions League Triumphfahrt FC Liverpool
Juergen Klopp kocha wa mabingwa wa Champions League msimu huu LiverpoolPicha: picture-alliance/dpa/B. Coombs

Liverpool tena  na  Napoli

"Napoli tena," sifahamu  sasa  ni  mara  ya  ngapi nakumbana  na Napoli, lakini  ni  timu bila  shaka  yenye  uzoefu  mkubwa," amesema kocha  wa  Liverpool  Juergen Klopp, ambaye amekumbana  na Wataliani  hao  akiwa  na  Dortmund katika  mwaka  2013-14  katika awamu  ya  makundi.

Liverpool inataraji kurejea katika fainali ya mwaka huu  ambayo itafanyika  Istanbul, ambako walishinda  taji lao la tano mwaka 2005.

Baada ya kushindwa katika  fainali  ya  msimu uliopita, Tottenham Hotspur inaweza kutarajia  kukutana na  mabingwa  wa  Ujerumani Bayern Munich katika  kundi B.

Huo utakuwa  mpambano wao wa kwanza  tangu  mwaka 1983-84 katika  kombe  la  UEFA. Watakutana pia  na  mabingwa  wa  Ugiriki Olympiakos  pamoja  na  Red Star  Belgrade ya Serbia, mabingwa wa  mwaka  1991 wa  kombe  la  Ulaya  la  washindi , katika  kundi B.

Baada  ya  kushinda  ligi  ya  Uropa , Chelsea wanarejea  katika Champions League  na  wana miadi  na  timu  iliyofikia  nusu  fainali msimu  ulipita katika  Champions League , Ajax pamoja  na  makamu bingwa  wa  champions League  wa  zamani  Valencia  pamoja  na Lille  ya  Ufaransa  katika  kundi H.

Manchester City Trainer Pep Guardiola
Pep Guardiola kocha wa Manchester CityPicha: picture-alliance/empics/PA Wire/M. Rickett

Mabingwa  wa  Premier League Manchester City wamepewa  kundi laini  miongoni  mwa  timu zote  wawakilishi  wa England  katika Champions League, ambapo vijana  wa  Pep Guardiola watapambana  na  Atalanta  Bergamo  ambao  ndio  kwanza wanaionja  Champions League pamoja  na  Shakhtar Donestsk na Dinamo Zagreb  katika  kundi C.

City iliishinda Shakhtar mabao 3-0 nchini  Ukraine  katika  awamu  ya makundi  msimu  uliopita  kabla  ya  kuikandika  mabao 6-0 katika mchezo wao  wa  mwisho.

Real na  PSG

Kutakuwa  na  mapambano  mengine  ya  kupendeza  kati ya wapinzani wanaofahamiana  kwingineko, ambapo kikosi  cha Zinedine Zidane cha  Real Madrid kitarejesha  mahusiano  ya kufahamiana  na  Paris  Saint-Germain  katika  kundi A. Real iliwaondoa  mabingwa  hao  wa  Ufaransa  katika  awamu  ya  timu 16 zilizobakia  katika  champions league  katika  njia  yao  kuelekea uibngwa  wao  misimu miwili iliyopita.

Real Madrid Trainer Zinedine Zidane
Kocha wa Real Madrid Zinedine ZidanePicha: picture-alliance/empics/M. Rickett

Mabingwa wa Uturuki Galatasaray  na  Club Brugge  ya  Ubelgiji wanakamilisha  kundi A. Cristiano Ronaldo na Juventus Turin watakabiliana  na  Atletico Madrid  tena  baada  ya  kukiangusha kikosi  hicho  cha  Uhispania katika  awamu ya timu 16 msimu uliopita.

Pia  watapambana  na  Bayer Leverkusen  na  Lokomotiv Moscow katika  kundi D.

Pengine sehemu  ambayo  ina uwiano  mzuri inazikutanisha  Zenit saint Petersburg , Benfica , Lyon na RB Leipzig  ambazo zitapambana  katika  kundi G. Michezo  ya kwanza  ya  makundi  yote itafanyika  Septemba 17 na 18.