1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kwanini Afrika inazongwa na maandamano ya vijana?

Josephat Charo Okeri Ngutjinazo
31 Julai 2024

Kote barani Afrika vijana wamekuwa msitari wa mbele wa maandamano, wakiwa hawaridhishwi na hali ya sasa ya kimaisha na uongozi. Nchini Nigeria maelfu ya watu wanaandamana kupinga ughali wa maisha na uchumi mbovu.

https://p.dw.com/p/4iyFV
Kenia | Proteste gegen Steuererhöhungrn in Nairobi
Picha: LUIS TATO/AFP/Getty Images

Katika miezi ya hivi karibuni Nigeria imeshuhudia maandamano ya hapa na pale, ukiwemo mgomo wa chama cha wafanyakazi uliovuruga usafiri wa anga na kusababisha umeme kupotea katika maeneo mengi. Hata hivyo, maandamano yanayotarajiwa kufanyika kote nchini yanatarajiwa kuwa makubwa kabisa kushuhudiwa tangu maandamano ya mwaka 2020 yaliyoshinikiza juhudi zifanyike kuutokomeza ugonjwa wa Sars chini ya #ENDSars.

Maandamano ya leo yaliyoandaliwa kwa kiwango kikubwa na vijana, yameungwa mkono kwenye mitandao ya kijamii kutumia hashtag "EndBadGovernanceinNigeria - tokomeza utawala mbovu Nigeria" na "RevolutionNow."- mapinduzi sasa. Wanadai kwamba serikali ya Rais Bola Tinubu ashughulikie magumu yanayosababishwa na njaa na uchumi. 

Nigeria yakabiliwa na kitisho cha maandamano wiki hii

Makundi ya vijana wa Nigeria yametiwa moyo na matukio ya hivi karibuni nchini Kenya, ambako vijana wa vuguvugu la Gen Z walimshinikiza Rais William Ruto alifute kazi baraza lake lote la mawaziri na kufuta muswada wa sheria ya fedha ulionuia kuongeza kodi na ambao haukuungwa mkono na Wakenya wengi. Kasi hii pia iliwahimiza vijana katika nchi jirani ya Uganda wafanye maandamano ya muda mfupi. 

Wanigeria hawatiliwi maanani

Nigeria | Lagos
Raia wa Nigeria waandamana dhidi ya ughali wa maisha Picha: SAMUEL ALABI/AFP

"Kama kuna nchi ulimwenguni ambayo watu wamepuuzwa kwa sababu ya uvumilivu wao basi Nigeria ni namba moja," ndivyo alivyosema Dakta Ibrahim Baba Shatambaya, mchambuzi na mhadhiri katika chuo kikuu cha Usma Danfodiya huko Sokoto. 
Shatambaya ameiambia DW kwamba tabaka la viongozi na watawala waliitumia migawanyiko ya kijamii miongoni mwa umma kwa muda mrefu ili kuendelea kuwadhibiti, hata hivyo hali ya kutoridhika na upinzani unaoongezeka nchini Nigeria umeendelea kudhihirika kwa watu.

Shatambaya aidha alisema mbinu hizi zinaonekana zimefeli safari hii na watu wanaitaka serikali ichukue hatua na iwajibike. 
Wanigeria mara kwa mara wameukosoa uamuzi wa serikali kufuta ruzuku ya mafuta iliyokuwa imepangwa muda mrefu. Kufutwa kwake kumesababisha ongezeko kiasi la gharama za maisha. Wengi wanalalamika kwamba masaibu yao yametokana na mageuzi yaliyoanzishwa tangu rais Tinubu alipoingia madarakani Mei 2023. 

Jeshi la Nigeria laonya dhidi ya ghasia za mtindo wa Kenya

Kinaya ni kwamba Tinubu alikuwa na jukumu muhimu katika maandamano ya mwaka 2012 ya Occupy Nigeria, yaliyoipinga hatua ya serikali ya rais Goodluck Jonathan kufuta ruzuku ya mafuta. Sasa, meza zimepinduliwa na toauti na Jonathan, rais Tinubu anajikuta yeye mwenyewe akiwa chini ya shinikizo. Amekuwa mara kwa mara akisisitiza kwamba kufuta ruzuku ya mafuta ni muhimu kuinusuru nchi hiyo kwenda muflis. 

Taasisi ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa, IMF, zenye makao yao makuu nchini Marekani, zimesema hatua hizo zilihitajika kuufufua uchumi wa Nigeria. 

Viongozi wa Nigeria wanataka kuyazuia maandamano

Nigeria | Bola Ahmed Tinubu
Rais wa Nigeria Bola Ahmed TinubuPicha: Sunday Aghaeze/AP Photo/picture alliance

Maafisa nchini Nigeria wamewahimiza vijana wasishiriki maandamano yoyote. Baadhi ya maafisa wa vyeo vya juu wamewatuhumu waandaaji wa maandamano hayo kwa uhaini na kwa kutaka kuiyumbisha nchi. 
Gavana wa jimbo la Ogun Mwanamfalme Dapo Abiodun aliwatahadhirisha vijana dhidi ya kuandamana na kuitisha pawepo mazungumzo na serikali kutafuta suluhisho la muda mrefu kwa matatizo ya Nigeria.

Hata hivyo kiongozi wa upinzani, Atiku Abubakar wa chama cha Peoples Democtaric alisisitiza kwamba serikali lazima itoe ulinzi kwa maandamano ya amani. Abubakar aliandika kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa X kwamba "Jitihada yoyote ya kuzibana haki hizi sio tu kinyume na katiba bali pia ni shambulizi la moja kwa moja la demokrasia yetu."

Mamilioni ya Wanigeria walala gizani kufuata mgomo wa taifa

Mwandishi wa DW, Shehu Salmanu, alisema makundi ya vijana yamewafahamisha polisi wa Nigeria na mawakala wote wa usalama na hakuna kurudi nyuma kwao katika azma yao ya kutaka kuingia mabarabarani kuandamana leo Agosti mosi. Salmanu pia amesema ni mojawapo ya ishara kwamba vijana wa Nigeria wanahaha na kutapa wakitaka madai au shida zao zitafutiwe ufumbuzi.